IMETHIBITIKA kuwa watu tisa wamekufa na wengine 12 hawajulikani waliko huku wengine 64 wakiokolewa baada ya boti ya abiria waliyokuwa wakisafiria katika Ziwa Tanganyika kuzama baada ya kukumbwa na dhoruba. Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Kigoma, Fraiser Kashai aliyekwenda eneo la tukio, alithibitisha jana kwamba boti hiyo iitwayo Tunusuru Yarabi iliyokuwa ikitoka Kirando, Rukwa kwenda Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) kupitia Rumonge, Burundi, ilikuwa na shehena ya dagaa, vyakula na bidhaa za viwandani. Kamanda Kashai alisema hadi jana mchana miili ya watu wanane kati ya tisa iliyokuwa imeopolewa ilikuwa imetambuliwa na kati yao, saba ikiwa ya wanawake na miwili ya watoto wa kiume ambayo imehifadhiwa katika hospitali ya mkoa ya Maweni. Aliwataja marehemu hao kuwa ni: Shani Baba wa Kirand, Mzinga Kandoro , Mwalimu wa Shule ya Msingi Filbert Bayi ya Dar es Salaam, Wamjini kutoka Burundi na Sarah Joseph wa Karundu, Nkasi, Rukwa. Wengine ni Nuru Hassan wa Kirando, Rukwa;