TFF YAANDAA KOZI YA MAKAMISHINA WA MPIRA WA MIGUU



TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

KOZI YA MAKAMISHNA WA MPIRA WA MIGUU
Kozi ya makamishna wapya kwa ajili ya Ligi Kuu ya Vodacom, Ligi Daraja la Kwanza, Ligi ya Taifa na Kombe la Taifa itafanyika ukumbi wa Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam kuanzia Agosti 6-8 mwaka huu.
Kwa wanaotaka kuwa makamishna ni lazima washiriki katika kozi ambapo ada ni sh. 10,000. Washiriki wanatakiwa kuwa waamuzi wastaafu na viongozi (administrators) wa mpira wa miguu katika ngazi mbalimbali. Pia wanatakiwa kuwasilisha vyeti vyao halisi (original) vya elimu.
Kutakuwa na mitihani ya kuandika ya sheria za mpira wa miguu na picha (video clips) ambapo watakaofaulu watapata vyeti.
Kwa upande wa makamishna waliopo sasa wa Ligi Kuu, wao watahudhuria kozi hiyo kwa siku moja (Agosti 8 mwaka huu). Kozi itaanza saa 2 asubuhi hadi saa 11 jioni. Washiriki wote wanatakiwa kujitegemea kwa usafiri, chakula na malazi kwa muda wote wa kozi hiyo.
Wakufunzi wa kozi hiyo watakuwa Kapteni mstaafu Stanley Lugenge, Joseph Mapunda na Leslie Liunda.
FAINALI LIGI YA TAIFA
Ligi ya Taifa hatua ya fainali inaanza kesho (Agosti 6 mwaka huu) kwenye Uwanja wa Mkwakwani jijini Tanga ikishirikisha timu 12 zilizogawanywa katika makundi matatu ya timu nne. Timu ya kwanza kutoka kila kundi na washindwa bora wawili (best losers)- watafanya jumla ya timu tano zitakazopanda Daraja la Kwanza.
Kundi A lina timu za Polisi Morani (Arusha), Mgambo Shooting (Tanga), Samaria (Singida) na Kasulu United (Kigoma). Polisi Dar es Salaam(Ilala), Majengo (Dodoma), Sifapolitan (Temeke) na Small Kids (Rukwa) ziko kundi B wakati kundi C lina timu za Mlale JKT (Ruvuma), Geita Veterans (Mwanza), Shinyanga United (Shinyanga) na Cosmopolitan (Ilala).
Kila siku zitachezwa mechi mbili ambapo katika ufunguzi kesho mchana Samaria itaumana na Kasulu United wakati jioni ni Polisi Morani na Mgambo Shooting.
Agosti 7 mwaka huu ni Sifapolitan na Small Kids wakati mchezo wa jioni utawakutanisha Polisi Dar es Salaam na Majengo.
Boniface Wambura
Ofisa Habari
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF)

Comments

Popular posts from this blog

PATA UKWELI KUHUSU MWANAMALUNDI, MTU WA MAAJABU ALIYEWAHI KUTOKEA KATIKA HISTORIA YA KABILA LA KISUKUMA