PPRA Yafungia Makampuni 7 Kwa Udanganyifu, Yatoa Ripoti ya Mwaka




Mwenyekiti wa Bodi ya PPRA, Balozi Matern Lumbanga


Mwenyekiti wa Bodi ya PPRA, Balozi Matern Lumbanga (Kulia) akiongea na waandishi wa habari, Kushoto ni Afisa Mtendaji Mkuu wa PPRA, Dk. Laurent Shirima.







Mamlaka ya Ununuzi wa Umma (PPRA), imeyafungia makampuni 7 pamoja na wakurugenzi wake kutokana na vitendo vya udanganyifu.
Akizungumza na waandishi wa habari leo katika makao makuu ya PPRA, Mwenyekiti wa Bodi ya PPRA, Balozi Matern Lumbanga amesema kuwa Mamlaka hiyo imeamua kuyafungia makampuni hayo kwa mujibu wa kifungu cha 62 cha Sheria ya Manunuzi ya Umma Na. 7 ya Mwaka 2011 na Kanuni ya 98 ya Tangazo la Serikali Na. 446 la Mwaka 2013.


Aidha, Balozi Lumbanga alisema kuwa kati ya makampuni hayo, Gagaja Contractors Company Limited, limefungiwa kwa kipindi cha miaka 10 (kutoka tarehe 2 Oktoba,2015 hadi 1 Octoba, 2025) kwa kosa la kuwasilisha dhamana za zabuni za kughushi wakati wa michakato ya zabuni.

Aidha, Balozi Lumbanga alisema kuwa makampuni mengine Sita yamefungiwa kwa kipindi cha miaka miwili (kuanzia tarehe 2, Oktoba, 2015 hadi 1, Oktoba 2017 kwa kukiuka masharti ya mikataba.

Makampuni hayo sita ni pamoja na Intersystem Holdings Company Limited,PEMA TECH Company Limited, Nyakire Investment Limited, Kosemwa Prospects Company Limited, PERNTELS Company Limited na Car and General Trading Limited.

Katika hatua nyingine, PPRA imetoa matokeo ya ukaguzi ya mwaka wa fedha 2014/2015 ambapo imebainika kuwepo kwa ongezeko kidogo la uzingatiaji wa sheria katika manunuzi ya umma.
“Matokeo yamebaini kiwango kidogo cha ongezeko la uzingatiaji wa sheria kutoka wastani wa asilimia 65 mwaka jana hadi kufikia asilimia 69 mwaka huu. Aidha, wastani huu bado uko chini ya lengo lililowekwa la asilimia 75,” alisema Balozi Lumbanga.

Aidha, alibainisha kuwepo mapungufu kadhaa ikiwa ni pamoja na malipo hewa ya kazi za ujenzi wa kandarasi katika taasisi 9, malipo yenye thamani ya zaidi ya shilingi milioni 951.7.
“Malipo ya zaidi ya shilingi milioni 951.7 yalilipwa kwa wakandarasi kwa kazi hewa (non existing works). Kiasi hiki ni sawa na asilimia 15 ya jumla ya thamani ya miradi yote ya kazi za ujenzi iliyokaguliwa,”alisema.
Kadhalika, ripoti hiyo ilibainisha uwepo wa viashiria vya rushwa katika baadhi ya taasisi na kueleza kuwa Mamlaka hiyo itayapeleka majina ya taasisi hizo TAKUKURU kwa ajili ya uchunguzi.

Alizitaja taasisi hizo kuwa ni NEC (29%), Halmashauri ya Manispaa ya Kinondoni (21), Halmashauri ya Wilaya ya Mpanda (22%), Halmashauri ya Wilaya ya Kibondo (24%), Halmashauri ya Wilaya ya Kigoma (28%), Agricultural Input Trust Fund (28%), Halmashauri ya Wilaya ya Mbozi (20%) na Halmashauri ya Wilaya ya Karatu (31%).

Comments

Popular posts from this blog

PATA UKWELI KUHUSU MWANAMALUNDI, MTU WA MAAJABU ALIYEWAHI KUTOKEA KATIKA HISTORIA YA KABILA LA KISUKUMA