Wizara ya Elimu yapanga kuwa Dodoma kwa awamu kati ya Agosti 15 na Septemba 15


WIZARA ya Elimu, Sayansi na Teknolojia imesema imejipanga kuhakikisha inahamia Dodoma kabla au ifikapo Agosti 15 mwaka huu.

Kumekuwa na hekaheka kwa taasisi na wizara mbalimbali za umma kuhamia Dodoma ili kuunga mkono tamko la Rais John Magufuli ambaye Jumamosi ya wiki iliyopita aliuahidi Mkutano Mkuu Maalumu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) kuwa Serikali yake itatekeleza ndoto ya siku nyingi ya Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere ya kuhamia katika mji mkuu huo.

Jana Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia imekuwa ya tatu kutangaza kuhamia Dodoma baada ya ile ya Kilimo, Uvuvi na Mifugo na Wizara ya Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu.

Wizara hizo zinaitikia wito wa Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa ambaye alitangaza kuhamia Dodoma ifikapo Septemba mwaka huu huku akiwataka mawaziri kumfuata.

Tangazo lililotolewa na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kwa watumishi wake limeeleza kuwa Wizara hiyo itahama kwa awamu mbili.

Awamu ya kwanza ambayo itatakiwa iwe imehamia Dodoma ifikapo Agosti 15 mwaka huu, itahusisha idara na vitengo vipatavyo tisa.

Kwa mujibu wa tangazo hilo vitengo au idara zitakazohusika ni pamoja na Idara ya Utawala na Rasilimali watu, Idara ya sera na mipango.

Nyingine ni Idara ya Elimu ya Juu, Idara ya Elimu ya Ufundi na Mafunzo ya Ufundi Stadi. Kwa upande wa vitengo vitakavyohusika ni pamoja na Kitengo cha Ununuzi na Ugavi, Kitengo cha Ukaguzi wa Ndani, Kitengo cha Sheria, Kitengo cha Habari na Kitengo cha Tehama (ICT).

Tangazo hilo pia limebainisha kuwa awamu ya pili ya kuhamia Dodoma itakuwa ni ifikapo Septemba 15, mwaka huu na itahusisha idara na vitengo vitatu.

“Ofisi ya kamishna wa elimu, Kitengo cha fedha na uhasibu, Kitengo cha uratibu wa elimu kikanda na kimataifa,” linasomeka tangazo hilo.

Comments

Popular posts from this blog

PATA UKWELI KUHUSU MWANAMALUNDI, MTU WA MAAJABU ALIYEWAHI KUTOKEA KATIKA HISTORIA YA KABILA LA KISUKUMA