KAMANDA MALISA GODLISTEN,AONYESHA NIA YA DHATI YA KULITETEA JIMBO LA MOSHI VIJIJINI KWA KUKOSA MBUNGE WA KULISEMA KWA MIAKA 10

MOSHI VIJIJINI INANIHITAJI - MALISA.!


Kamanda Malisa akirudisha fomu

UTANGULIZI:
Kwa takribani miaka 10 sasa jimbo la Moshi Vijijini limekuwa "iddle" kutokana na kukosa mbunge wa kulisemea. Mbunge aliyepo Dr.Cyril Chami aliteuliwa kuwa Naibu Waziri na baadae Waziri muda mfupi tu baada ya kuchaguliwa (kabla hajaachwa nje ya baraza).
Nafasi ya uwaziri imemfanya Chami ashindwe kuwajibika vizuri kwa wananchi wake, kwa sababu akiwa kama Mbunge hawezi kuiwajibisha serikali ambayo yeye ni sehemu yake (Nemo judex in causa sua).
Changamoto za Moshi vijijini ni nyingi, hivyo ni dhahiri jimbo hili linamhitaji mtu shupavu anayeweza kulitetea kwa "nguvu ya hoja" na "hoja za nguvu" ktk kusukuma mbele gurudumu la maendeleo.
KWANINI NAOMBA RIDHAA YA KUGOMBEA;
Kabla sijatangaza azma hii nilijiuliza sana maswali mengi na kushirikisha watu wangu wa karibu kunishauri.
Lengo ni kuwa sikutaka lengo langu langu la kuomba ridhaa ya kugombea lichukuliwe tofauti na dhamiri yangu inavyonituma. Kwenye uchaguzi huu watu wengi sana hasa vijana wametangaza nia ya kugombea kupitia vyama mbalimbali.
Wapo wenye dhamira ya kweli ya kuwatumikia wananchi ila hawa ni wachache, wengi wapo kwa malengo binafsi. Wengine kulinda biashara zao, wengine ili walipwe mishahara mikubwa na kuishi maisha ya kifahari, wengine ili kupata ajira maana hawana ajira so wamechukulia ubunge kama "kick" ya kutokea kimaisha.
Changamoto iliyopo ni kumtambua yupi ana dhamira ya kweli ya kuwatumikia wananchi na yupi anatafuta ajira au ana malengo binafsi. Na hapa ndipo vyama vya siasa vinapaswa kuwa na busara sana kuhakikisha vinampata mgombea sahihi.
Binafsi nimesukumwa na dhamira ya kweli ya kuwatumikia watu. Dhamira hii ya uongozi ni ya kuzaliwa (charisma) kwani nimekuwa kiongozi tangu ningali kinda kama historia yangu inavyoonesha.
Kama ni Kazi ninayo kazi nzuri inayonipa fursa ya mshahara mzuri, usafiri, nyumba, na fursa nyingine. Pia nje ya kazi ninafanya ujasiriamali unaoniwezesha kuongeza kipato. Hivyo dhamira yangu ya kugombea haijasukumwa na maslahi binafsi.
KWANINI MOSHI VIJIJINI.
Awali nilipanga kugombea Udiwani wa kata ya Kiboriloni. Lakini nikapata fursa ya kukutana na viongozi wa chama (wiki chache zilizopita) ambao walinishauri kusitisha mpango huo kwa sasa kwa sababu mbalimbali.
Sababu mojawapo ni kuwa Mhe.diwani aliyepo sasa ndugu Frank Kagoma ni mchapakazi hodari licha ya kukalia kiti cha udiwani kwa miezi michache tu hadi sasa. Katika kipindi cha chini ya mwaka mmoja tangu achaguliwe, Kagoma ameweza kusimamia miradi mingi ya maendeleo ikiwemo ujenzi wa soko la kisasa la bidhaa ambalo limejengwa kwa ufadhili wa Mhe.Philemoni Ndesamburo, Mbunge wa Moshi mjini (japo CCM hawataki wananchi kutumia soko hili).
Miradi ya maji, maboresho ya elimu, ujenzi wa maabara, kuimarisha ulinzi wa watu na mali zao ni baadhi ya mambo yanayompa Kagoma "legitimacy" ya kuendelea kuwatumikia watu wa Kiboriloni. Kama ameweza kufanya yote haya kwa kipindi kisichozidi mwaka mmoja tangu achaguliwe ni dhahiri akipewa muda zaidi anaweza kufanya makubwa zaidi.
Baada ya kusitisha mpango wa udiwani Kiboriloni nimejipima na kuona ninaweza kuwakilisha vizuri wananchi wa Moshi (V).
Hivyo basi nilifika Moshi na kuchukua fomu ya kuomba ridhaa ya chama kupitishwa kama Mgombea wa jimbo hilo. Nilipata mapokezi mazuri ikiwa ni pamoja na kuchangiwa gharama za fomu na wananchi wenyewe. Baada ya kuijaza fomu hiyo niliirejesha ofisini kwa hatua nyingine za kichama.
ELIMU:
1. Nina Shahada ya Mawasiliano ya Umma (B.A in Mass Communication, chuo kukuu SAUT, TZ), 2013,
2. Nina Astashahada ya utawala ktk sekta ya Afya (Health Management &Promotion, PHCI & Johns Jopkins University,
USA), 2014
3. Na Kwa sasa nasoma Stashahada ya Sheria na Maadili ktk sekta ya Afya (Dipl.In Medical Law and Ethics, ALISON & JHU, USA online study).
UZOEFU KATIKA UONGOZI.
1. Nimekua Rais wa serikali ya wanafunzi chuo kikuu cha St.Augustine mwaka 2012 hadi 2013.
2. Nimekuwa Mwenyekiti wa umoja wa wanafunzi vyuo vikuu kanda ya ziwa (LAZOHLISU), mwaka 2013.
3. Nimekuwa Katibu Mkuu wa Shirikisho la wanafunzi vyuo vikuu Katoliki Tanzania (Students' Union of Catholic Universities in Tanzania, zamani SUSAUT), mwaka 2012 hadi 2013.
4. Nimekuwa Mratibu kanda (Regional Coordinator) wa Shirikisho la vyuo vukuu Afrika Mashariki (East African Community Students' Union) chini ya sekretarieti ya Haki za binadamu na utawala bora.
5. Mjumbe wa Baraza la Fikra la vijana wa Aftika Mashariki (The East Africa Youth Think Tank), kuanzia mwaka 2014 hadi sasa.
6. Mjumbe Jumuiya ya Vijana wataaluma wa nchi za kusini mwa Afrika (SADC Young Profesionals Association), kuanzia February mwaka huu hadi sasa.
7. Pia nimeendelea kushika nafasi mbalimbali za uongozi katika taasisi mbalimbali ikiwemo ujumbe wa Bodi ktk taasisi ya kusaidia watoto waishio ktk mazingira magumu ya Victorious Foundation.
UZOEFU KATIKA SIASA.
Kabla sijajiunga na CHADEMA (July 2007) nilikua Mkereketwa na mfuasi wa Sera, Falsafa na Itikadi ya chama hiki kwa muda mrefu hivyo baada ya kujiunga nimeweza kushika nafasi mbalimbali kama ifuatavyo;
1. Mjumbe wa Mkutano Mkuu wa Wilaya/Jimbo kupitia Kata ya Kiboriloni kuanzia mwaka 2009 - 2012.
2. Katibu Uenezi wa CHADEMA Tawi la Chuo Kikuu cha St.Augustine (CHASO SAUT) kuanzia mwaka 2011 hadi 2012.
Pia nimeweza kushiriki shughuli na 'operations' mbalimbali za chama kama ifuatavyo;
1. Kuhamasisha na kushawishi upiga kura ktk uchaguzi mdogo Arumeru mwaka 2012.
2. Kuratibu ziara za CHADEMA tawi la SAUT katika kutoa Elimu ya Uraia kwenye maeneo mbalimbali ya kanda ya Ziwa, hususani Geita, Sengerema na Shinyanga, 2011 & 2012.
3. Kuratibu na kufanikisha ziara za viongozi mbalimbali wa chama jijini Mwanza, kama vile Dr.Slaa (2011), na Tundu Lissu (2012).
4. Kushiriki kikamilifu katika uchaguzi mdogo wa Kalenga nikiwa kama mwangalizi huru nikisimamia kata za Tosamaganga, Tanangozi na Ifunda.
UANDISHI;
Pia nimeweza kuandika makala mbalimbali za kuelezea sera za CHADEMA na kuikosoa serikali ya CCM na utawala wake. Makala zangu ni miongoni mwa makala zinazojipatia umaarufu mkubwa kwa watumiaji wa mitandao ya kijamii.
Baadhi ya makala maarufu nilizowahi kuandika ni pamoja na;
1. MTOTO WA MKULIMA AMEANZA KUPOTEZA IMANI, MwanaHalisi 2009.
2. MWONGOZO WA SPIKA NI "MSUKULE" WA CCM, unpublished, 2011.
3. KINYAGO TULICHOKICHONGA WENYEWE KIMEANZA KUTUTISHA, Social Media, 2013.
4. UKISTAAJABU YA UHAMIAJI UTAYAONA YA UTUMISHI, social media 2014
5. CCM WANAPENDA NAMBA LAKINI HAWAJUI HESABU, Nipashe, June 2015.
VIPAUMBELE;
Ikiwa chama changu kitanipa ridhaa ya kusimama kama mgombea nitasimamia Ilani ya chama, lakini pia nitahakikisha natekeleza yafuatayo;
1. MAJI; Jimbo Moshi Vijijini ni miongoni mwa Majimbo yenye vyanzo vingi vya maji lakini bado wananchi wake wanapata shida ya maji. Ukiondoa maji ya JR mfumo wa idara ya Maji umeshindwa kuwa na tija Moshi vijijini.
Hivyo nitahakikisha vyanzo vyote vya maji vilivyopo maeneo mbalimbali kama Kidia, Materuni (Uru), Kibosho na maeneo mengine vinaboreshwa na kuwezesha upatikanaji wa maji mengi yatakayokidhi mahitaji ya wananchi wote wa Moshi vijijini waishio milimani na wale wa Maeneo ya Tambarare kama Mabogini na Chekereni.
2. BARABARA; Barabara zote za Moshi Vijijini zinapaswa kuwa kwa kiwango cha lami kabla ya mwaka 2020 kwa kutumia rasilimali za ndani. Kwa mfano mwaka 2013 sekta ya utalii ilichangia pato la taifa jumla ya Dola Bil.4.4 (kwa mujibu wahttps://en.m.wikipedia.org/wiki/Tourism_in_Tanzania). Hii ni takribaliTrilioni kumi kwa exchange rate ya leo.
Katika pesa hizo Mlima Kilimanjaro ulichangia dola Bil.1.2 takribani Shilingi Trilioni 3, Na ndio sekta ya utalii iliyochangia kiasi kikubwa zaidi ukilinganisha na maeneo mengine kama Mbuga za wanyama, Utalii wa fukwe, mapango ya kale, etc.
Watalii waliopanda kwa kupitia njia zilizopo Moshi Vijijini walichangia takribani dola Mil.150 yani Shilingi Bilioni 400. Kungekua na utaratibu angalau 10% ya fedha hizi kuingia kwenye mfuko wa jimbo au Halmashauri basi kwa mwaka 2013 jimbo lingepata Bilioni 40 kutoka Mlima Kilimanjaro.
Pesa hizi zingeweza kutumika kuweka lami barabara 2 au 3 za jimbo. Gharama ya kuweka lami za kiwango kizuri ni takribani Sh.Bilioni 1.2 kwa kilomita moja. Kwa hiyo Bilioni 40 kwa mwaka zingetosha kuweka lami barabara ya Old-Moshi Kidia yenye urefu wa kilomita 10, na barabara ya Matindigani yenye kilomita 8, na kumalizia kipande cha barabara ya Kibosho (Umbwe) na barabara nyingine ambazo bado hazina lami. Mwaka unaofuata tukipata Bil.40 nyingine tunaendelea na barabara nyingine. Baada ya miaka mitano barabara zote za jimbo zitakua na lami. Tunaweka rekodi ya kuwa jimbo pekee la vijijini ambalo barabara zake zote ni za lami.
3. UJENZI WA MABWENI/HOSTELS SHULENI; Mojawapo ya mambo yanayofanya kuporomoka kwa kiwango cha elimu Moshi Vijijini ni watoto kutembea umbali mrefu na kukosa muda wa kutosha wa kujisomea. Licha ya ujenzi wa shule za kata lakini kuna vijiji vipo zaidi ya kilomita 10 ndani ya kata moja na hivyo kuwa changamoto kwa mtoto kufika shuleni.
Kwa mfano mwanafunzi anayesoma Sekondari ya Komakya akitokea kijiji cha Lyakombila anatembea zaidi ya kilomita 13 kwenda na 13 kurudi licha ya kuwa shule hiyo na kijiji viko kata moja. Hali kadhalika kwa baadhi ya maeneo kama Mloe Omarinyi na Dakau Chini (Kibosho).
Hivyo kama Mbunge nitahakikisha kupitia mfuko wa jimbo, wafadhili mbalimbali na wadau wa elimu tunajenga Hostel za kutosha kwenye kila shule ya kata ili kupunguza umbali mrefu kwa wanafunzi na kuhakikisha wanapata elimu bora.
Nitaifanya Moshi Vijijini kuwa jimbo la kwanza nchini kuwa na hostels za kisasa kwenye shule zote za kata. Ikumbukwe Moshi Vijijini ndio jimbo la kwanza kujenga shule za kata kabla hata ya mpango huo kuanzishwa. Wakati shule za kata zinaanzishwa mwaka 2006, Moshi vijijini walikua na shule za Kata tangu mwaka 1995. Hivyo basi kama tuliweza kuwa wa kwanza kwenye ujenzi wa shule za kata, tutakuwa wa kwanza kujenga hostels kwa shule zote za kata jimboni.
4. KUBUNI VYANZO VIPYA VYA MAPATO NA KUKUZA PATO LA JIMBO;
Kama Mbunge nitahakikisha kunakua na vyanzo vipya vya mapato ili kuwezesha wananchi kujiajiri na kuondoa utegemezi wa kuajiriwa. Maeneo nitakayotilia mkazo ni Kilimo, viwanda vidogovidogo (hasa vya bidhaa za mbao, ushonaji, Uhunzi, etc).
Nitahakikisha kunakuwepo na soko la uhakika la bidhaa zitokanazo na mazao ya kilimo kwa wananchi wa Moshi vijijini. Wananchi wengi wameng'oa kahawa baada ya kuona haina tija. Wanalima kwa gharama kubwa kisha wakivuna wanakopwa kahawa yao na vyama vya ushirika na hawalipwi hela zao kwa wakati. Mimi nitakua mwarobaini wa tatizo hili. Nitapigania soko la uhakika kwa mazao yote ya kilimo hasa kahawa, na kumaliza migogoro iliyopo kati ya wakulima na vyama vya Ushirika.
5. KUBORESHA BARABARA ZA KUPANDISHA WATALII;
Nitahakikisha barabara zote zinazopandisha watalii Mlima Kilimanjaro zilizopo jimboni kwangu zinaboreshwa na kuwa na uhakika wa kupitika kipindi chote cha mwaka.
Pia niahakikisha barabara zilizokua zikitumika kupandisha watalii Mlima Kilimanjaro zamani, zinarudi katika utoaji huduma. Mojawapo ni barabara ya ya Old Moshi Kidia ambayo ilikua ikitumika zamani lakini kwa sasa TANAPA wamezuia.
Ikumbukwe hii ndio barabara fupi zaidi kupanda mlima Kilimanjaro kuliko barabara nyingine zote. Ina umbali wa kilomita 10 tu kutoka Moshi mjini hadi geti la KINAPA, ukilingsnisha na barabara nyingine kama ya Marangu (kilomita 39.5, Rongai kilomita 108, au Machame kilomita 42).
Ufunguzi wa barabara hii utawafanya watalii wengi zaidi kuja Tanzania na hivyo kufungua fursa za kiuchumi kama biashara ya utalii, hoteli, na makampuni ya utalii.
Ufunguzi wa barabara hii utaenda sambamba na kuboresha barabara nyingine zinazotumika kupandisha watalii mlima Kilimanjaro ziwe katika viwango vya kimataifa. Mojawapo ni barabara ya Kibosho Mweka ambayo watalii hutumia kushukia.
Kwa mujibu wa mtandao wawww.prweb.com/releases/2013/3/prweb10559544.htm mwaka jana 2013/2014 idadi ya watalii waliopanda Mlima Kilimanjaro walikuwa 52000. Hii inamaanisha barabara zaidi zikifunguliwa watalii zaidi watapanda. Idadi ya watalii itaongezeka na pato litokanalo na utalii litaongezeka pia.
6. UANZISHWAJI WA BENKI YA WANANCHI;
Nitakua chachu ya upatikanaji wa mikopo yenye masharti nafuu kwa vijana ili kuwezesha kujiajiri.
Ili kutimiza hili nitashawishi uanzishwaji wa benki ya Wananchi (Moshi Community Bank) ambayo itaendeshwa na wananchi wenyewe kwa mtaji utakaotokana nao wenyewe na kuongezewa na wahisani na wafadhili mbalimbali.
Wastani wa pato la mwananchi wa Moshi Vijijini ni takribani Shilingi Milioni moja na nusu hadi mbili kwa mwaka (kwa mujibu wa bodi ya taifa ya takwimu). Hiki ni kiwango kikubwa zaidi ukilinganisha na pato la mwananchi wa Ludewa kwa mwaka ambalo ni wastani wa shilingi laki 3 hadi laki 5 kwa mwaka.
Hii ni kusema kuwa tumewazidi Ludewa mara nne. Lakini wananchi wa Ludewa wana benki yao wenyewe, benki ya wananchi (Ludewa Community Bank) inayosaidia kwenye shughuli mbalimbali za maendeleo ikiwa ni pamoja na kutoa mikopo yenye masharti nafuu. Kama Ludewa wameweza sisi pia tunaweza. Na atakayewezesha hayo ni Malisa si mwingie.!
Hayo ni kwa uchache lakini mengi zaidi nitayasema ikiwa chama kitanipa ridhaa ya kugombea.
ILI KUPATA MOSHI VIJIJINI MPYA TUNAHITAJI MTU MPYA MWENYE FIKRA MPYA NA MBINU MPYA.

Comments

Popular posts from this blog

PATA UKWELI KUHUSU MWANAMALUNDI, MTU WA MAAJABU ALIYEWAHI KUTOKEA KATIKA HISTORIA YA KABILA LA KISUKUMA