TWANGA KUSUGUA KISIGINO MBEYA NA IRINGA.



Bendi ya muziki wa Dansi ya African Stars maarufu kama Twanga Pepeta iliyo na maskani yake jijini Dar, inatarajiwa kufanya ziara maalum katika mikoa ya Iringa na Mbeya ili kuwashukuru mashabiki wa mikoa hiyo miwili kutokana na kuipigia kura kwa wingi na kufanikiwa kuchukua tuzo tatu za KILI kwa mwaka huu.

Ziara hiyo inatarajiwa kuanzia katika Mkoa wa Iringa siku ya Alhamisi ya tarehe 3 mwezi wa sita katika Club ya V.I.P, na siku inayofuata ya tarehe 4 mwezi wa sita Twanga pepeta itamalizia ziara yake katika ukumbi wa Mkapa uliopo katikati ya Jiji la Mbeya.

Maonyesho yote mawili yanatarajia kuanza saa mbili za usiku na kwa Mkoa wa Iringa, Twanga pepeta inataraji kusindikizwa na Bendi ya Sweat Noise iliyo na maskani yake Iringa.

Twanga pepeta itaitumia ziara hiyo ya mikoa ya Iringa na Mbeya kuwadhihirishia mashabiki wa Mikoa hiyo kwamba Twanga Pepeta iko juu na wanataraji kusafiri na kikosi kizima kilicho na nyota wote wakiongozwa na Kiongozi Mkuu mamaa Luiza Mbutu na wengineo kibao.

Aidha kwa kuwa Twanga toka izindue Albamu ya Mwana Dar es salaam haijawahi kufanya ziara katika Mikoa hiyo wanataraji kuzipiga live nyimbo zote zilizo kwenye albamu hiyo sambamba na wanamuziki wapya wa Bendi hiyo waliojiunga toka Bendi pinzani za FM ACADEMIA na DIAMOND MUSICA ambao ni SEIF TUMBA anayepiga Tumba, Allain Kisso anayekunguta gitaa la Solo wengine ni Mpiga drums Mussa Kambangwa, wanenguaji ni pamija na Queen Suzy, Asha Sharapova, Sabrina Mathew na Said.

twanga pepeta ambayo kwa sasa inatamba na staili yao mpya ya SUGUA KISIGINO wanataraji kuutambulisha mwimbo wao mpya uliotungwa na Kiongozi msaidizi Saleh Kupaza.

Ziara ya Twanga Pepeta kwa mikoa ya Iringa na Mbeya imeandaliwa kwa pamoja na Kampuni ya Tasha Promotion na ASET chini ya uratibu wa Jimmy Tasha.

Comments

Popular posts from this blog

PATA UKWELI KUHUSU MWANAMALUNDI, MTU WA MAAJABU ALIYEWAHI KUTOKEA KATIKA HISTORIA YA KABILA LA KISUKUMA