SERIKALI IMENUNUA MASHINE MPYA YA CT-SCAN KATIKA HOSPITALI YA TAIFA YA MUHIMBILI

Na Magreth Kinabo –MAELEZO
Serikali imenunua mashine mpya ya CT-Scan yenye thamani ya takriban dola za Marekani milioni 1.7 yenye uwezo wa hali ya juu kwa ajili ya kutoa huduma za uchunguzi wa magonjwa mbalimbali katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili(MNH) iliyopo jijini Dar es Salaam.
Ununuzi wa mashine hiyo, umefanyika kufuatia agizo la Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli aliyoifanya hivi karibuni ambapo aliutaka uongozi wa hospitali hiyo kuboresha huduma zake na kuhakikisha vifaa tiba na dawa vinapatikana ili kuhakikisha Watanzania wanapata huduma bora za afya.
Hayo yamegundulika leo baada ya Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Dkt. Hamisi Kingwangala aliyoifanya leo katika hospitali hiyo, ambapo alitembea Idara ya Magonjwa ya Dharura,Idara ya Mionzi, sehemu mpya ya wagonjwa waliopo chini ya ungalizi maalum(ICU), ambayo inafanyiwa ukarabati na wodi mojawapo.
Naibu Waziri akitembelea katika Idara ya Mionzi ambapo alijionea mashine za MRI na CT –Scan zinavyofanyakazi.
Akizungumzia kuhusu mashine ya CT-Scan Mkuu wa Idara ya Mionzi, Dkt. Flora Lwakatare alisema mashine hiyo , iliyotengenezwa na kampuni ya Siemens mpya imefungwa siku mbili zilizopita na imeshaanza kufanya majaribio kwa wagonjwa 26 tangu ilipofungwa
Dkt. Flora aliongeza kwamba mashine hiyo iko moja tu nchini na katika nchi za Afrika Mashariki nchi nyingine iliyonunua mashine hiyo ni Kenya katika Hospitali ya Aghakhan.
“ Mashine hii inatoa huduma za hali ya juu kwa magonjwa ya moyo, ubongo tumbo kifua na inauwezo wa kupima kifua na tumbo kwa sekunde sita,” alisema.
Akizungumzia kuhusu mashine hiyo Naibu Waziri huyo, alisema imenunuliwa kwa fedha za Serikali wala sio mkopo.
“Tunatarajia kununua mashine hii katika hospitali ya Dodoma na Mwanza,” alisema Waziri Kingwangala.
Kwa upande wake Kaimu Mkurugenzi wa MNH, Profesa Laurence Maseru alisema mashine hiyo ina sahani 128 mara 2 ikilinganishwa na iliyokuwepo ambayo ilikuwa inatumia sahani sita.
Kwa upande wa mashine ya MRI ambayo tangu ilipofanyiwa matengenezo makubwa Novemba 26, mwaka jana hadi sasa imesha hudumia wagonjwa 560.
Dkt. Kingwangala alitembea katika Idara cha huduma za dharura na kuangalia jinsi huduma zinavyotolewa, ambapo alielezwa na Mkuu wa Idara ya Magonjwa ya Dharura Dkt. Juma Mfinaga alisema ambayo huhudumia wastani wa wagonjwa 300 hadi 400 kwa siku ambacho kinafanya kazi kwa kutumia mfumo maalum wa kompyuta bila kutumia karatasi.
Naibu Waziri huyo, mbali na kupongeza maboresho yaliyofanyika na huduma nzuri, alitoa maagizo kwa uongozi wa hospitali hiyo kuboresha huduma za zilinazotolewa hospitalini kuwa za kitaifa zaidi.
Alitolea mfano huduma kulipa kwa kuongeza vitanda na matumizi ya choo kimoja kila chumba ili kuweza kuvutia wateja.
“Sisi tunaweza kufanya biashara kwa kuboresha huduma za kulipa ili zimpendeze na kuvutia wateja. Na fedha zitakazopatikana zitatumika kununua dawa , vifaa tiba na kuwapatia wafanyakazi motisha, alisema.
Aliutaka uongozi huo pia kuhakikisha inawalipa wafanyakazi fedha za malipo ya ziada kwa wakati ifikapo tarehe 25 ya mwezi unaofuata,kutumia mfumo wa kompyuta sehemu zote, kupunguza msongamno wa wagonjwa na kuwa wabunifu.(P.T)

Comments

Popular posts from this blog

PATA UKWELI KUHUSU MWANAMALUNDI, MTU WA MAAJABU ALIYEWAHI KUTOKEA KATIKA HISTORIA YA KABILA LA KISUKUMA