Maafisa walivyojikanganya mbele ya Rais Magufuli alipokagua ghafla JNIA


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akikagua mashine ya ukaguzi wa mizigo katika sehemu ya kuwasili abiria ya uwanja wa ndege wa Mwalimu Julius Nyerere, upande wa uwanja wa zamani (Terminal One) wakati wa ziara yake ya ghafla aliyoifanya Ijumaa tarehe 13 Mei, 2016. Kulia kwa Rais ni Mkuu wa Mkoa wa Dar es salaam Paul Makonda na kushoto ni Kaimu Meneja uendeshaji Lilian Minja.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli ameiagiza Wizara ya Ujenzi, Mawasiliano na Uchukuzi kwa kushirikiana na vyombo vya dola kuchukua hatua mara moja dhidi ya dosari za ukaguzi zilizopo katika kitengo cha ukaguzi wa mizigo na abiria katika uwanja wa ndege wa kimataifa wa Mwalimu Julius Nyerere (Terminal One) Jijini Dar es salaam.

Rais Magufuli ametoa agizo hilo leo tarehe 13 Mei, 2016 alipofanya ziara ya kushtukiza katika uwanja huo na kubaini kuwa mashine za ukaguzi za sehemu ya kuwasili abiria na mizigo hazifanyi kazi kwa muda mrefu.

Maafisa wa uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Mwalimu Julius Nyerere waliokuwa wakitoa maelezo juu ya hali ya kitengo cha ukaguzi wa mizigo na abiria katika uwanja huo, walikuwa wakitoa taarifa zinazotofautiana kuhusu utendaji kazi wa mashine za ukaguzi, hali iliyosababisha Dkt. Magufuli aamue kuiagiza wizara husika kwa kushirikiana na vyombo vya dola kuchukua hatua mara moja.

"Unajua mimi sipendi kudanganywa, ni vizuri uzungumze ukweli tu, kwa nini nimeanzia hapa huwezi ukajiuliza? eeeh sasa sipendi kudanganywa, ukinidanganya nitachukia sasa hivi, wewe umenidanganya kwamba hiyo ndio mbovu na hii ndio nzima, nikawaambia muiwashe hiyo nzima, akaja huyu mwenzako amezungumza ukweli kabisa, akasema hii ni mbovu kwa miezi miwili. Dkt. Magufuli aliwahoji Maafisa wa uwanja wa ndege.

"Kwa hiyo mizigo inayoingia humu huwa hamuikagui kwa namna yoyote ile, kwa hiyo mtu nikiamua kuja na madawa yangu ya kulevya, nikaja na dhahabu zangu, na almasi zangu na meno ya tembo kwa kutumia hizi ndege ndogondogo napita tu" Rais Magufuli aliendelea kuwabana maafisa hao wa uwanja wa ndege wa kimataifa wa Mwalimu Julius Nyerere. 

Rais Dkt. John Pombe Magufuli amefanya ziara hii ya kushtukiza mara baada ya kuwasili katika uwanja wa ndege wa Mwalimu Julius Nyerere akitokea Jijini Kampala nchini Uganda ambako jana alihudhuria sherehe ya kuapishwa kwa Rais wa Jamhuri ya Uganda Mhe. Yoweri Kaguta Museveni.

Gerson Msigwa
Kaimu Mkurugenzi wa Mawasiliano,
IKULU
Dar es salaam

13 Mei, 2016



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akimuuliza maswali Meneja wa Uwanja wa ndege wa Mwalimu Julius Nyerere Bw. Paul Rwegasha, kuhusu dosari zilizopo katika mashine za kukagulia mizigo ya wageni wanaowasili kupitia uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Mwalimu Julius Nyerere, upande wa uwanja wa zamani (Terminal One)

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akiwabana maswali maafisa wa uwanja wa ndege wa kimataifa wa Mwalimu Julius Nyerere kuhusu dosari ya kutofanya kazi kwa mashine za ukaguzi katika sehemu ya kuwasili abiria ya uwanja wa zamani (Terminal One) .

Comments

Popular posts from this blog

PATA UKWELI KUHUSU MWANAMALUNDI, MTU WA MAAJABU ALIYEWAHI KUTOKEA KATIKA HISTORIA YA KABILA LA KISUKUMA