Shy-Rose Bhanji Amwonya Msekwa

KADA wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Shy-Rose Bhanji, amemshutumu Makamu Mwenyekiti wa CCM (Bara), Pius Msekwa na kumtaka aache kukifanya chama hicho kama mali yake.
Shy-Rose ambaye aliwania ubunge katika Jimbo Kinondoni, jijini Dar es Salaam na kushindwa kwenye kura za maoni, alitoa kauli hiyo jana akijibu kauli ya Msekwa ya juzi akiwataka wanaotaka kuhama chama hicho baada ya kushindwa kwenye uteuzi wahame haraka.
Akizungumza na Tanzania Daima Jumatano kwa njia ya simu, Shy-Rose alisema ameshtushwa na kauli ya Msekwa kwani hakuwa na haki ya kutamka maneno mazito na yasiyo ya kiungwana hasa katika kipindi hiki cha kuelekea Uchaguzi Mkuu.
“Kwa kweli nilivyosoma gazeti moja leo nimekutana na habari hii, ikanishtua kidogo. Nikajiuliza hivi huyu mzee Msekwa anasema maneno ya ajabu namna hii, hiki chama ni chake binfasi? Pengine amejisahau kwamba CCM ni chama chetu wote, sasa iweje yeye awe na ujasiri wa kujiamini kutoa maneo ya ajabu wakati hiki ni chama chetu wote au yeye anadhani ni chama chake?” alihoji Shy-Rose.
Shy-Rose alisema anaheshimu nafasi ya Msekwa kama kiongozi wa juu wa chama na vile vile kama mzazi wake, lakini nafasi hiyo haimpi uhalali wa kushabikia wanachama wanaotaka kuondoka kwenye chama hicho.
Alisema Msekwa alipaswa kujiuliza kwa nini wanachama hao wanaondoka na si kuzungumza maneno ambayo yanaonyesha wazi kwamba yana jazba ndani yake.
“Huu si wakati wa jazba, huu ni wakati wa kutafakari kwa nini watu wanaondoka CCM. CCM kazi yetu ilikuwa kupokea wapinzani, leo wanaondoka, lazima tujiulize hilo” alisema.
Kada huyo ambaye ni mjumbe wa Halmashauri Kuu ya Mkoa wa Dar es Salaam na mjumbe wa Baraza Kuu la (UWT) Taifa, aliwataka viongozi wa CCM kwa sasa kuchunga kauli zao, vinginevyo hawatapata ushindi unaotarajiwa.
Alikumbushia uchaguzi mdogo wa ubunge Tarime, mkoani Mara mwaka juzi kwamba CCM ilishindwa kutokana na kauli za majigambo ya baadhi ya viongozi wa chama.
Akizungumzia msimamo wake baada ya kushindwa kwenye kura za maoni, Shy-Rose alisema hana mpango wa kuhama CCM kwa sasa.
“Kama kuondoka CCM, aondoke Msekwa na atuachie chama chetu, yeye hana mamlaka wala uhalali wa kuzungumza lugha za ajabu ambazo zitawafanya hata wale wasio na nia ya kuhama waondoke.
“Mimi sihami CCM, nimekulia ndani ya chama hiki na nitaendelea kubaki ndani ya chama lakini pale nitapoona kuna kasoro sitasita kukikosoa chama changu na nitasema kweli daima,” alisema.
Aliwapongeza walioamua kuondoka CCM kwani wametumia haki yao na kusisitiza kwamba kuondoka CCM si dhambi kama ambavyo wengine wanavyofikiria.

habari hii ni kutoka website ya
http://www.kishoka.com

Comments

Popular posts from this blog

PATA UKWELI KUHUSU MWANAMALUNDI, MTU WA MAAJABU ALIYEWAHI KUTOKEA KATIKA HISTORIA YA KABILA LA KISUKUMA