Rapa matawi ya juu wa Bendi ya Akudo Impact ‘Vijana wa Masauti’, Emmanuel Kalonji ‘Toto Ze Bingwa’, anasakwa na Vijana wa Mwema (Polisi) kwa tuhuma za kumshushia kipigo Rapa mwenzake, Kanal Top na kumvunja mkono.

Tukio hilo lilitokea hivi karibuni ndani ya Ukumbi wa Adventure Mjini Moshi wakati Bendi hiyo ilipokuwa huko kwa ajili ya shoo ya Mkesha wa Pasaka.

Chanzo chetu cha kuaminika kililitonya Ijumaa kuwa, awali Kanal Top alionekana akipanda stejini kufanya makamuzi kabla ya kushuka chini kumpisha rapa mwenzake Toto Ze Bingwa kuendeleza libeneke ambapo naye baadaye alishuka na kumpisha Kanal Top tena.

Ikadaiwa kwamba, wawili hao waliendelea na kupishana kwa staili ya ‘anza wewe, nitafuata’, lakini mwishowe Kanal Top alimalizia kuchana mistari kisha kushuka chini.

Ikazidi kudaiwa kuwa, wakati Kanal akishuka chini alipokelewa na rafiki yake mmoja wa huko Arusha na kuanza kupiga naye stori ambapo ghafla alitokea Toto Ze Bingwa na kuanza kumchimba mkwara kuwa atamfanyia kitu mbaya.

“Jamaa kusikia hivyo ikabidi ahoji inakuwaje, mara akashangaa anaambulia kipigo kikali na kusukumwa kisha kuanguka chini na kuvunjika mkono,” alisema mtoa habari wetu aliyeomba hifadhi ya jina lake.

Ikaelezwa kwamba, baada ya tafrani hiyo jamaa alikimbizwa katika moja ya hospitali iliyopo mkoani humo kabla ya kuhamishiwa katika Hospitali ya Muhimbili kwa matibabu zaidi ambapo alifungiwa Mhogo ‘POP’.

Baada ya taarifa hiyo kutua mezani kwetu, Mwandishi wa Ijumaa alimvutia waya Kanal Top kuzungumzia tukio hilo ambapo alikiri na kueleza kuwa alilazimika kuliripoti tukio hilo katika Kituo cha Polisi cha Oysterbay, jijini Dar na kufunguliwa jalada la kesi lenye namba RB/OB/5996/010 Shambulio la kudhuru mwili. Ze Bingwa anatafutwa.Habari hii ni kwa hisani ya
www.globalpublisher.com

Comments

Popular posts from this blog

PATA UKWELI KUHUSU MWANAMALUNDI, MTU WA MAAJABU ALIYEWAHI KUTOKEA KATIKA HISTORIA YA KABILA LA KISUKUMA