KITILA MKUMBO AWASHUKURU ACT KWA KUMPENDEKEZA KUWANIA URAIS

Aliyeteuliwa kuwania urais kupitia chama cha ACT Wazalendo, Kitila Mkumbo.
Ndugu Wazalendo,
Naomba niwashukuru nyote kwa imani kubwa mliyo nayo juu yangu katika kukiwakilisha chama katika nafasi ya Rais. Naishukuru pia Kamati Kuu kwa imani yake kwangu hata kufikia hatua ya kupitisha azimio la kuniomba nigombee urais kwa chama chetu. Jana Kamati Kuu ilituma ujumbe maalumu nyumbani kwangu kwa ajili ya kuzungumza na familia na jamaa zangu juu ya ombi hili.
Aidha, Nimekuwa nikilitafakari jambo hili tangu Alhamisi nilipoombwa rasmi kutafakari uwezekano wa mimi kugombea baada ya juhudi zetu za kutafuta mgombea kushindikana. Nimefanya mawasiliano mapana katika familia, ndani ya chama, chuoni ninapofanyia kazi, Kanisani kwangu,na kwa watu na taasisi mbalimbali ninazohusiana nazo.
Baada ya tafakari na mawasiliano (consultations) mapana nasikitika kusema kwamba sina utayari na maandalizi ya maana ya kisaikolojia, kifamilia, na kisiasa kuniwezesha kugombea nafasi ya urais katika uchaguzi huu.
Najua nimewaangusha sana katika uamuzi wangu huu lakini naamini kwamba mtaheshimu uamuzi wangu na kwamba hamtaacha kuthamini mchango wangu katika chama kwa sababu ya kukataa kugombea urais.
Nasikitika kwa tuhuma ambazo baadhi ya wanachama wetu wanarusha katika mitandao ya kijamii na sehemu zingine. Nathamini na kuheshimu haki ya wanachama wetu kuonyesha hasira kwa jambo wasilolipenda. Hata hivyo nawasihi wanachama wetu wajizuie kuzusha mambo yatakayochochea chuki ndani ya chama na kukatishana tamaa.
Nashauri tuwaombe wanachama wetu wengine waandamizi wachukue jukumu hili, wakiwemo mama mwenyekiti na Katibu Mkuu, kuwataja tu kwa uchache.
Tunapotafari haya, tusisahau Malengo Mapana ya chama chetu tuliyojiwekea katika uchaguzi huu. Ni bahati nzuri kwamba tumefanikiwa kuweka wagombea wa ubunge na Udiwani katika kata na katika majimbo mengi. Tusiyumbe.
Ahsanteni.
Kitila Mkumbo
17 Agosti 2015

Comments

Popular posts from this blog

PATA UKWELI KUHUSU MWANAMALUNDI, MTU WA MAAJABU ALIYEWAHI KUTOKEA KATIKA HISTORIA YA KABILA LA KISUKUMA