Utapeli wa nyumba za kupanga waibuka


Chanzo:mwananchi
By Mwandishi Wetu, Mwananchi
 
Dar es Salaam. Umeibuka mtandao wa matapeli jijini hapa wanaojifanya madalali wa nyumba na viwanja, ambao wanatumia matangazo na namba za simu wanazoziweka magazetini kuwanasa watu kwa urahisi. 
Mtandao huo wa matapeli unaoongozwa na mtu anayejifanya kuwa ni daktari katika Hospitali ya Amana na mmiliki wa nyumba moja inayopangishwa iliyopo Mtoni Kijichi. Polisi inamsaka mtu huyo baada ya kumtapeli mkazi mmoja wa Temeke.
Akisimulia juzi namna alivyoangukia mikononi mwa mtandao huo na kutapeliwa Sh1.4 milioni za kodi ya nyumba, mfanyakazi wa Mamlaka ya Elimu Tanzania (Tea), Tito Mganwa alisema alikuwa akitafuta nyumba ya kupanga, ndipo alipopiga simu za madalali alizoziona kwenye gazeti moja la kila siku (siyo Mwananchi).
Mganwa alisema baada ya kupiga namba hizo, aliambiwa kuwa daktari mmoja anayefanya kazi katika Hospitali ya Amana anatafuta mpangaji kwenye nyumba yake iliyopo Mtoni.
Alisema kwa kuwa alikuwa akihitaji kupata nyumba haraka, alikutana na madalali hao na kwenda kuonyeshwa nyumba hiyo na kumkuta mlinzi aliyewatembeza ndani ya nyumba.
Baada ya kuvutiwa na mazingira ya nyumba yalivyo, Mganwa alimwambia mwenye nyumba kwa njia ya simu kuwa atalipa kodi ya miezi sita kwa awamu mbili; awamu ya kwanza Sh1.4 milioni.
“Tulikubalina tukutane pale Hospitali ya Amana, ambako anafanya kazi, nilikwenda na kumkabidhi fedha mkononi. Nikiwa palepale alijifanya anampigia simu mlinzi na kumwambia afanye usafi nyumba kwa vile tayari nilishalipa kodi,” alisema Mganwa.
Mganwa alisema baada ya kulipa alikwenda kwenye nyumba ile ili kuifanyia usafi, ndipo aliposhangazwa kusikia kuwa mlinzi hakuwa amepigiwa simu kama mwenye nyumba alivyoagiza.
Alisema alikwenda kituo cha polisi kuandikisha maelezo na kupewa RB ya kuwakamata matapeli hao, kisha aliambatana na polisi hadi kwenye nyumba hiyo, lakini hawakumkuta mlinzi.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Temeke, Andrew Satta alimtaka Mganwa kwenda ofisini kwake ili msako wa kumtafuta mwenye nyumba hiyo ufanyike na pia kujua kama kuna matukio mengine yamehusisha nyumba hiyo.

Comments

Popular posts from this blog

PATA UKWELI KUHUSU MWANAMALUNDI, MTU WA MAAJABU ALIYEWAHI KUTOKEA KATIKA HISTORIA YA KABILA LA KISUKUMA