PAC YAAGIZA WASIRA AONDOLEWA KWENYE NYUMBA ANAYOISHI

Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC), imeiagiza Bodi ya Sukari Tanzania (SBT) kumwondoa katika nyumba ya bodi hiyo, Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais (Mahusiano na Uratibu), Stephen Wasira kutokana na kuishi katika nyumba hiyo kinyume na taratibu.

Wasira akiwa Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika alikuwa akiishi katika nyumba hiyo inayomilikiwa na SBT iliyopo Masaki jijini Dar es Salaam.

Mkurugenzi Mtendaji wa SBT, Henry Semwaza aliieleza Kamati ya PAC jana katika kikao kilichofanyika kwenye ofisi ndogo za Bunge jijini Dar es Salaam, kuwa wamekuwa wakifanya jitihada za kuwasiliana na Wasira kuhusu kuirejesha nyumba hiyo, lakini hakuna utekelezaji wowote unaofanyika.

“Mara ya mwisho tulimwandikia barua mwaka 2012 kuhusu kuirejesha nyumba hiyo, lakini bado hajairejesha na anaendelea kuishi katika nyumba hiyo,” alisema Semwaza.

Mwenyekiti wa PAC, Zitto Kabwe akitoa azimio la Kamati hiyo alisema, “Hapa hakuna msukumo mnaoufanya yaani tangu mwaka 2012 mlipomwandikia barua mpaka sasa kimya. Tunaiagiza SBT kumwandikia barua Wasira mkimtaka arejeshe nyumba na nakala ya barua hiyo tuipate Jumatatu (Januari 19 mwaka huu).”

Alisema kutokana na kuwapo kwa harakati za kutaka kubadili hati ya umiliki ya nyumba hiyo, Zitto alisema, “Msajili wa Hazina kamati inakuagiza uhakikishe umiliki wa nyumba hiyo unabaki kwa bodi ya sukari na si vinginevyo.”

Zitto pia alimwagiza Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo, Chakula na Ushirika, Sophia Kaduma amwandikie barua Katibu Mkuu Kiongozi kuhusu uamuzi huo wa Kamati.

Pia, PAC imeishauri Wizara ya Kilimo kuandaa sheria itakayounda Bodi ya Sukari isiyokuwa na mgongano wa kimaslahi ili kutoa fursa ya kufanya uamuzi tofauti na ilivyo sasa.

Comments

Popular posts from this blog

PATA UKWELI KUHUSU MWANAMALUNDI, MTU WA MAAJABU ALIYEWAHI KUTOKEA KATIKA HISTORIA YA KABILA LA KISUKUMA