RAIS KENYATTA ATAKIWA KUFIKA ICC



Mahakama ya kimataifa ya Jinai ICC, inamtaka Rais Uhuru Kenyatta kufika Hague tarehe 8 mwezi Oktoba. Hii ni licha ya majaji wanaotarajiwa kusikiliza kesi dhidi yake kuiahirisha.

Kesi dhidi ya Kenyatta ilitarajiwa kuanza Oktoba tarehe 7.
Katika taarifa ya mahakama hiyo, kutakuwepo na mikutano miwili ya hadhara kujadili hali ya ushirikiano kati ya kiongozi wa mashitaka na serikali ya Kenya kuhusiana na kesi hiyo. 

Swala hilo liliibuka katika taarifa ya kiongozi wa mashitaka iliyotolewa Septemba tarehe 5.
Katika taarifa yake, mahakama imesema kuwa mwakilishi wa Rais Kenyatta atahitajika kuhudhuria mkutano wa kwanza huku Rais Kenyatta akitakiwa kuhudhuria mkutano wa pili utakaojadili hali ya kesi yake.

Vikao hivyo viwili, vitashirikisha kiongozi wa mashitaka, upande wa utetezi na mawakili wanaowawakilisha waathiriwa wa ghasia za baada ya uchaguzi mkuu mwaka 2007/08.

Taarifa hiyo ilisema kuwa mahakama iliamua kuahirisha kesi dhidi ya Kenyatta ili kujipatia muda zaidi kutafakari maombi yaliyotolewa na pande zote kwenye kesi hiyo bila ya kuonea au kupendelea upande wowote.
Rais Kenyatta ameshitakiwa kwa kuhusika na ghasia za baada ya uchaguzi nchini Kenya mnamo mwaka 2007/08.

Anakabiliwa na makosa matano ya kutenda uhalifu dhidi ya binadamu ikiwemo mauaji, kuwalazimisha watu kuhama makwao , ubakaji na vitendo vingine vinavyokwenda kinyume na haki za binadamu.

Inadaiwa yote hayo aliyafanya wakati wa ghasia za baada ya uchaguzi mkuu mwaka 2007-2008.

Comments

Popular posts from this blog

PATA UKWELI KUHUSU MWANAMALUNDI, MTU WA MAAJABU ALIYEWAHI KUTOKEA KATIKA HISTORIA YA KABILA LA KISUKUMA