MINJA AACHIWA KWA DHAMANA NA KUAGIZWA AWAAMBIE WAFANYA BIASHARA WAFUNGUE MADUKA

01 Apr 20




Mwenyekiti wa Wafanyabiashara nchini, Johnson Minja ameachiwa kwa dhamana na serikali imeambiwa isisikie maneno ya kuambiwa.

Mwenyekiti huyo ambaye alifutiwa dhamana Machi 26, alirejeshwa mahakamani leo ambapo kesi yake ilitajwa, akitokea gereza la Isanga.

Kwa mujibu wa mahakama ya mkoa wa Dodoma, kesi hiyo itaanza kusikilizwa kwa maelezo ya awali Aprili 9 mwaka huu kutokana na ushahidi wa kesi hiyo kukamilika.

Machi 5, mwaka huu, Mahakama ilimuonya mshitakiwa huyo kuacha kuwashawishi wafanyabiashara nchini kuacha kufunga maduka yao na kwenda kusikiliza kesi yake kila inapotajwa.

“Moja ya sharti la dhamana yako ni kuhakikisha kuwa unaendeleza amani wakati wote wa kesi yako ikiwa ni pamoja na kuwaambia wafanyabiashara waendelee kufungua maduka yao ili wananchi waendelee kupata huduma, kwa nini umewaambia wafanyabiashara wafunge maduka yao?” 
alihoji hakimu Mbilu.

Hata hivyo Minja alijibu kuwa hana taarifa zozote za wafanyabiashara nchini kufunga maduka.

Wafanyabiashara hao walisema wanasuburi leo kama mwenyekiti huyo ataachiwa tena kwa dhamana ili waendelee na biashara kwani wengi wao wana mikopo ya benki na wamekaa wiki nzima bila kufanya biashara.

Awali, habari ifuatayo iliripotiwa:

UMATI mkubwa wa Wafanyabiashara Nchini, umekusanyika katika jengo la mahakama amjini hapa kusikiliza kesi ya mwenyekiti wao Johnson Minja inayounguruma leo.

Mwandishi wetu aliyepo mahakamani amesema pamoja na umati huo kuna ulinzi mkali huku watu wote wakiwa wamezuiwa kuingia eneo la mahakama kabla ya kesi kuanza.

Minja ambaye atakuwa anatokea rumande ya Isanga kuja kusikiliza kesi yake amesababisha nchi kutetemeka kutokana na maduka mengi hasa makubwa kufungwa kushinikiza aachiwe kwa dhamana.

Aidha, jana Bunge lilipiga kelele kuhusiana na suala hilo na kutaka serikali kumtoa mwenyekiti huyo ili kuendelea na mazungumzo kuhusu kodi na namna ya kulipa bila kukiuka Katiba.

Minja alifutiwa dhamana Machi 26, mwaka huu kutokana na kukiuka masharti ya dhamana aliyopewa. Dhamana ya mshitakiwa huyo ilitenguliwa kutokana na kile kinachodaiwa na mahakama kushindwa kwake kuwazuia wafanyabiashara kutofunga maduka wakati kesi yake inapoendelea hali inayowasababishia wananchi adha kubwa ya kukosa huduma kinyume na masharti ya dhamana aliyopewa Januari 28 mwaka huu wakati alipofikishwa mahakamani kwa mara ya kwanza.


Kesi hiyo inasikilizwa mbele ya Hakimu Mkazi wa mahakama ya mkoa wa Dodoma, Rebecca Mbilu.

  • Taaarifa hii imenukuliwa kutoka kwenye blogu ya Beda Msimbe, Lukwangule

Comments

Popular posts from this blog

PATA UKWELI KUHUSU MWANAMALUNDI, MTU WA MAAJABU ALIYEWAHI KUTOKEA KATIKA HISTORIA YA KABILA LA KISUKUMA