Kauli za baadhi ya Mawaziri wateule wa baraza la Rais Magufuli


SAA chache baada ya kutangazwa kwa Baraza jipya la Mawaziri na Rais Dk. John Magufuli, MTANZANIA iliwatafuta baadhi ya mawaziri na kuzungumza nao kuhusu uteuzi wao.


BALOZI MAHIGA

Kwa upande wake, Waziri mteule wa Wizara ya Mambo ya Nje, Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Kikanda na Kimataifa, Balozi Dk. Augustine Mahiga, alisema: “Siwezi kuongea jambo lolote kwa sababu hata rais wangu hatujazungumza…nawaomba muwe na subira.

“Nikimaliza kuongea na rais, hata ninyi watu wa media (vyombo vya habari), nitakuwa na jambo la kuwaambia, nakushukuru ndugu mwandishi,” alisema Balozi Mahiga.

KITWANGA

Waziri mteule wa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Charles Kitwanga, alisema amefurahishwa na uteuzi huo, ambapo aliahidi kuhakikisha anasimamia ulinzi wa wananchi na mali zao.

“Sipendi kuzungumza sana kuhusu namna ambavyo nitatekeleza majukumu yangu kama Waziri wa Mambo ya Ndani, ila napenda kutoa salamu kwa wahalifu wote kuwa tutapambana nao kwa nguvu zote,” alisema.

ANGELINA MABULA

Naibu Waziri mteule wa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Angelina Mabula, alisema amejipanga kukabiliana na changamoto zilizopo katika wizara hiyo.

Akizungumza kwa njia ya simu, Mabula ambaye ni mbunge wa Ilemela, alisema wizara hiyo ina changamoto nyingi.

Alisema kuwa amepokea kwa furaha uteuzi huo na kumpongeza Rais Magufuli kutokana na kuwa na imani kubwa naye na kuahidi kuwatumikia Watanzania kwa nguvu zake zote.

“Nafahamu ugumu wa Wizara ya Ardhi, kuna kero ambazo zimekuwa zinawakabili Watanzania hasa masikini, kuna migogoro ya wakulima na wafugaji, nitahakikisha namsaidia rais kukabiliana na changamoto hizi kwa nguvu zote.

“Nimejiandaa kutumika kwa ajili ya Watanzania, nina uzoefu wa kutosha, hivyo natoa rai kwa watumishi wa wizara hiyo kutoa ushirikiano wao kwetu na kamwe hatutasita kuchukua hatua kwa wale ambao watashindwa kwenda na kasi ya Serikali ya awamu ya tano,” alisema.

MANYANYA

Akizungumza baada ya kutangazwa kuwa Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi, Mhandisi Stella Manyanya, alisema alipatwa na mshangao kusikia ameteuliwa kushika wadhifa huo.

“Nakiri wazi kuwa nimepatwa na mshangao mkubwa, nilikuwa sifikiri hata siku moja kwamba nitateuliwa kushika nafasi kama hii.

“Nawashukuru waliokaa chini na kuona nafaa, kwa sababu taifa hili lina watu wengi mno jamani. Namshukuru Mungu, wananchi wa jimbo langu, mkuu wa wilaya na viongozi wa halmashauri yangu (Nyasa) waliosimamia uchaguzi nikawa mbunge.

“Kumbe walikuwa na maono ya mbali… eeh Mungu wangu asante na awabariki wote,” alisema.

Alipoulizwa kama anaweza kwenda na kaulimbiu ya Rais Magufuli ya ‘Hapa Kazi Tu’, Mhandisi Manyanya alisema yuko tayari kuwatumikia Watanzania.

“Nipo tayari kwenda na kasi hii, unajua kaulimbiu hii inatuhamasisha mno kuchapa kazi, inatupa nguvu ya kuondokana na utendaji kazi wa mazoea, huu ndiyo moto wa kutimiza majukumu yangu.

UMMY MWALIMU

Waziri wa Afya na Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu, alisema amepokea uteuzi huo kwa heshima kubwa na unyenyekevu.

“Nimepokea uteuzi uliofanywa na Rais Dk. John Pombe Magufuli kwa heshima na unyenyekevu mkubwa. Nipo tayari kukabiliana na changamoto zinazoambatana na kazi hii ya Waziri wa Afya, Jinsia, Wazee na Watoto,” alisema Ummy.

MAVUNDE

Naibu Waziri mteule wa Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Kazi, Vijana na Ajira, Anthony Mavunde, alisema anahisi ana deni kubwa kwa taifa kutokana na uteuzi wake.

“Najisikia deni kubwa la kuwatetea wananchi kwa uadilifu na uaminifu mkubwa ili kumsadia Rais Magufuli. Nitawatumikia wananchi na Watanzania kwa uzalendo uliotukuka hasa kuhakikisha Tanzania inapiga hatua kimaendeleo,” alisema.

SIMBACHAWANE

Akizungumzia uteuzi wake, Waziri mteule wa TAMISEMI, Utumishi na Utawala Bora, George Simbachawene, alisema hana maoni yoyote ila kwake ni kazi tu.

“Maoni yangu ni hapa kazi tu, sina maoni yoyote zaidi ya hayo,” alisema Simbachawene.

ASHATU

Naibu Waziri mteule wa Wizara ya Fedha na Mipango, Dk. Ashatu Kijaji, alisema hawezi kuzungumzia kitu ambacho hakijui.

“Nipo kijijini sana na ‘network’ siyo nzuri sana, siwezi kuongea lolote, naweza nikawa najibu vitu ambavyo sivielewi, nitafute baadae,” alisema Dk. Kijaji.


RAIS wa Awamu ya Tano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. John Pombe Magufuli, ametangaza Baraza la Mawaziri na kumteua Mbunge wa Jimbo la Mtama, Nape Nnauye kuwa Waziri wa Habari, Utamaduni, Wasanii na Michezo.

Awali kabla ya uteuzi wa jana wa Serikali ya Awamu ya Tano, wizara hiyo ilikuwa chini ya mbunge wa kuteuliwa Dk. Fenella Mukangara na Naibu Waziri wake Juma Nkamia ambaye ni Mbunge wa Chemba.

Akitangaza baraza hilo jana jijini Dar es Salaam, Rais Magufuli alisema kutakuwa na jumla ya mawaziri 19 ndani ya wizara 18 ambapo baadhi hazitakuwa na Manaibu Waziri lengo likiwa ni kuwa na baraza dogo ili kupunguza gharama.

Nape ambaye pia ni Katibu wa Itikadi na Uenezi Taifa wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), kabla ya kuteuliwa kuwa waziri aliwahi kufanya mahojiano na MTANZANIA na kuwatoa hofu Watanzania wanaopenda michezo akiwataka wawe na imani na Rais wa Awamu ya Tano, akiamini ataweza kuinua michezo nchini tofauti na wanavyofikiria.

“Nawapa mfano, Rais wa Awamu ya Tatu, Benjamin Mkapa, hakuwahi kuwa mwanamichezo wala kuwahi kukanyaga uwanjani, ila ametuachia alama ya uwanja,” alisema.

Nape pia katika mazungumzo hayo na gazeti hili, hakusita kuzungumzia matokeo mabovu ya soka hivi karibuni ambapo alisema hayo yamesababishwa na kutowekeza katika soka badala yake tunatengeneza timu kiujanja ujanja.

“Tukitaka matokeo makubwa inatubidi tufanye uwekezaji ili tufanye vizuri, tusifanye vitu kirahisi Serikali lazima iwekeze lakini badala ya kuwekeza tunaanzisha vitu kirahisi Azam B, Yanga B na Simba B, ndio maana tunakutana na wachezaji wenye umri mkubwa lazima tukubali kuwekeza,” alisema Nape.

Alieleza kuwa kuna wakati yalifanyika makosa makubwa ambapo Waziri wa Elimu, Joseph Mungai, alifuta michezo shuleni jambo ambalo lilichangia kuua michezo kabisa lakini sasa michezo inatakiwa kurudi.

Alisema ili kufikia mafanikio, zitungwe sheria zitakazowabana watu, sheria zitakazoongeza maslahi ya wachezaji.

Nape pia alitaka zitungwe sheria za michezo ambazo zitasaidia kuwabana wanamichezo ambao wanatumia vilevi kama pombe na dawa za kulevya.

Hatua ya kuteuliwa kwake kuwa Waziri wa Michezo kunaweza kusaidia kupunguza machungu ya Watanzania waliokata tamaa kutokana na kufanya vibaya katika michuano mbalimbali ya kimataifa na kutekeleza hayo aliyoyaongea wakati wa mahojiano alipotembelea ofisi za New Habari (2006) Ltd, wachapishaji wa magazeti ya Mtanzania, Rai, The African, Bingwa na Dimba.

Comments

Popular posts from this blog

PATA UKWELI KUHUSU MWANAMALUNDI, MTU WA MAAJABU ALIYEWAHI KUTOKEA KATIKA HISTORIA YA KABILA LA KISUKUMA