Wapiganaji wa IS kuondoka kusini mwa Damascus



Kambi ya Yarmouk kusini mwa Damascus, kwa sasa inawahifadhi raia 7,000 wa Palestina na Syria.
Na RFI
Nchini Syria, makubaliano yaliowashangaza wengi yamefikiwa juu ya kuondoka Jumamosi hii kwa watu 4000 katika maeneo matatu kusini mwa mji wa Damascus.

Watu hao ni pamoja na wapiganaji wa kundi la Islamic State (IS), wapiganaji wa kundi la Al-Nusra Front na raia wa kawaida, vyanzo vilio karibu na mazungumzo vimebaini Ijumaa Desemba 25.

Hii ni mara ya kwanza kwa mkataba kama huu unaolishirikisha kundi la Islamic State. Mkataba huu unaruhusu watu 4000, ambao ni raia pamoja na wapiganaji hasa wa kundi la Islamic State na wale wa kundi la Al-Nusra Front, kuondoka katika kambi ya wakimbizi wa Palestina ya Yarmuk, kusini mwa mji wa Damascus, na maeneo jirani ya miji ya Qadam na Hajar al Aswad.

Kwa mujibu wa chanzo cha serikali ya Syria, utekelezaji wa makubaliano hayo unapaswa kuanza Jumamosi hii Desemba 26. Watu hawa 4000 watahamishiwa katika mji wa Raqqa, "mji mkuu" wa kundi la Islamic state, kaskazini mwa Syria, au katika mji wa Marea, katika jimbo la Aleppo, kwenye mpaka na Uturuki, unaoshikiliwa na makundi ya waasi wa Kiislam na kundi la Al-Nusra Front.

Kwa mujibu wa chanzo cha serikali ya Syria, kikosi cha askari kiliingia katika mji wa Qadam Alhamisi Desemba 24 ili kuchukua magari na vifaa vya kijeshi. Mabasi kumi na nane yamewasili katika eneo hilo na yako tayari kuwasafirisha. "Kila mpiganaji ataruhusiwa kuondoka pamoja na familia yake, sanduku moja na silaha yake binafsi", mwakilishi wa serikali katika eneo hilo amesema.

Siku za nyuma majaribio manne kama hayo yalishindikana, chanzo hicho cha serikali kimebaini. Kuondoka huko ni matokeo ya mazungumzo yalioanzishwa miezi miwili iliyopita kati ya serikali na wawakilishi wa wakazi wa maeneo matatu kusini mwa mji mkuu wanaosumbuliwa na kuzorota kwa kiasi kikubwa kwa hali ya maisha. Inaarifiwa kuwa hali hiyo imesababishwa na kuzingirwa kwa maeneo hayo na jeshi la serikali tangu mwaka 2013, shirika la Haki za Binadamu nchini Syria (OSDH) limebainisha.

Kambi ya Yarmouk inawahifadhi karibu raia 7000 wa Palestina na Syria, dhidi ya watu zaidi ya 160,000 kabla ya kuanza kwa machafuko mwaka 2011. Mwezi Aprili, Makundi ya Islamic State na Al-Nusra Front yalikua yaliiteka kambi hiyo kwa 60% kabla ya kurudi nyuma kwa 40% ya eneo hilo.

Comments

Popular posts from this blog

PATA UKWELI KUHUSU MWANAMALUNDI, MTU WA MAAJABU ALIYEWAHI KUTOKEA KATIKA HISTORIA YA KABILA LA KISUKUMA