Mkuu wa Mkoa Katavi asimamisha kazi watumishi 12 wa serikali



MKUU wa Mkoa wa Katavi, Dk Ibrahim Msengi
MKUU wa Mkoa wa Katavi, Dk Ibrahim Msengi
MKUU wa Mkoa wa Katavi, Dk Ibrahim Msengi amewasimamisha kazi maofisa waandamizi 11 wa Manispaa ya Mpanda akiwemo Mkurugenzi Mtendaji wake, Suleiman Lukanga kwa ukiukwaji wa sheria za manunuzi kwa kufanya ubadhirifu fedha zaidi ya Sh milioni 92.8.
Dk Msengi alieleza kuwa Lukanga na maofisa 11 wa Manispaa ya Mpanda wanatuhumiwa kununua gari la kubeba taka ambapo kiasi cha Sh milioni 92.8 zilitolewa kwa manunuzi hewa kwa kampuni hewa.
Wengine waliosimamishwa kazi ni Kaimu Mkurugenzi wa Manispaa hiyo, Vincent Kayombo ambaye pia ni Ofisa Elimu (Msingi) wa Manispaa ya Mpanda, Ofisa Manunuzi aliyetajwa kwa jina moja la Kakulima, Ofisa Mipango, Ferdinard Filimbi, Mweka Hazina, Bosco Kapinga, Mhasibu Kibi Hamis Msaka na wajumbe wanne wa Bodi ya Zabuni.

Dk Msengi ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Ulinzi na Usalama wa Mkoa huo, ameamuru wakati uchunguzi kuhusu tuhuma hizo ukiendelea, watuhumiwa wote 12 wasitoke nje ya Mji wa Mpanda na wahakikishe wanalipa kiasi hicho cha fedha kwa kuwa ni fedha za umma.

“Maofisa hawa wa Manispaa na Mkurugenzi wao wanatuhumiwa kufanya malipo hewa, ikiwa ni nusu ya fedha zilizotengwa kununua gari hilo hakika wamefanya kwa makusudi ..... “Sasa naomba watupishe ili tufanye uchunguzi kwa kuhusisha vyombo mbalimbali vya dola na wote wawe nje ya ofisi kuanzia sasa, lakini wasitoke nje ya Mji wa Mpanda.....naagiza pia walipe kiasi hicho cha fedha,” aliamuru.

Uamuzi huo umechukuliwa na mkuu huyo wa mkoa kutokana na uchunguzi uliofanywa na tume tatu tofauti zilizoundwa kuchunguza upotevu wa kiasi hicho cha fedha ambazo ni kati ya Sh milioni 200 zilizotolewa na Tamisemi kwa ajili ya kununulia gari la taka katika Manispaa ya Mpanda.

Aidha, Dk Msengi ametoa onyo kwa mtumishi yeyote aliyezoea kufanya ubadhirifu wa mali ya umma akisema wakae wakijua kuwa siku zao zimetimia na kwamba tabia hiyo ovu haiwezi kufumbiwa macho.

Katika uchunguzi wa upotevu huo wa kiasi hicho cha fedha uliofanywa na kamati tatu tofauti zilizoundwa na RC huyo zilibaini kuwa Kampuni ya Bluecyon iliyoko Mbezi, Dar es Salaam ilizawadiwa zabuni ya kununua gari hilo.

Uchunguzi wa Kamati hizo tatu zilizoongozwa na Katibu Tawala Mkoa, Polisi Mkoa na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) kuwa Bluecyon ilikuwa haijihusishi na biashara ya magari, bali ni kampuni ya uchapishaji.

Akizungumza mjini Mpanda, Lukanga alisema, “Nilikuwa kikazi kijijini baada ya kufika hapa mjini ndipo nimesikia agizo hilo la Mkuu wa Mkoa kwamba amewasimamisha kazi watumishi 12 wa Manispaa ya Mpanda nikiwemo na mimi niseme wazi kuwa agizo hilo tumelisikia.

“Hata kabla ya RC hajatoa taarifa hiyo jana tayari nilikuwa nimeanza kulishughulikia tangu mwaka jana na tayari baadhi ya watumishi wa Manispaa wamefikishwa mahakamani. Mgogoro unakuja baada ya mzabuni huyo kushindwa kuleta gari hilo la kubebea taka....basi nilichukua hatua ikiwemo kuvunja mkataba na mzabuni huyo na kuhakikisha fedha hizo zinarudi.
Chanzo:HabariLeo

Comments

Popular posts from this blog

PATA UKWELI KUHUSU MWANAMALUNDI, MTU WA MAAJABU ALIYEWAHI KUTOKEA KATIKA HISTORIA YA KABILA LA KISUKUMA