WATAKAOFANYA FUJO MKESHA WA MWAKA MPYA KUKIONA

Na Jacquiline Mrisho MAELEZO
Jeshi la Polisi Kanda maalum ya Dar es salaam limewatahadharisha wananchi kutokufanya fujo wakati wa mkesha wa mwaka mpya kwa kuweka mikakati mikali kwa watakaokaidi amri hiyo.
Akizungumza na Waandishi wa Habari leo Jijini Dar es salaam Kamishna wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es salaam Suleiman Kova amepiga marufuku uchomaji wa matairi ya gari, upigaji baruti, risasi za moto na fataki ambazo zaweza kusababisha madhara wakati wa mkesha wa mwaka mpya.
“ Ni baraka zaidi kusherekea sherehe kama hizi kifamilia na sio vizuri kuingia mwaka mpya ukiwa mahabusu, huo ni mkosi” Alisema Kamishna Kova.
Kamishna Suleiman Kova aliongeza kuwa watashirikiana na wadau mbalimbali ikiwa ni pamoja na Jeshi la Zimamoto, kampuni binafsi za ulinzi, vikundi vya ulinzi shirikishi pamoja na kutumia ndege za Polisi kufanya doria ili kuhakikisha kuwa wanailinda amani na kudhibiti aina yoyote ya uhalifu utakaojitokeza.
Aidha Kamishna Kova amesisitiza kuwa vituo vyote vya polisi vitakuwa wazi masaa 24 ili kuwawezesha wananchi kutoa taarifa haraka pindi wanapopata matatizo au wanapoona dalili zozote za uvunjifu wa amani pia amehakikisha kuwa fukwe zote za bahari na maeneo yote yenye mikusanyiko yatalindwa.
Katika kipindi hiki cha kuelekea mwisho wa mwaka wa 2015 Jeshi la Polisi Kanda Maalum ya Dar es salaam limetoa rai kwa wananchi kushirikiana na Jeshi hilo katika kuzuia uhalifu kwa kutoa taarifa haraka pindi waonapo dalili za uvunjifu wa amani.

Comments

Popular posts from this blog

PATA UKWELI KUHUSU MWANAMALUNDI, MTU WA MAAJABU ALIYEWAHI KUTOKEA KATIKA HISTORIA YA KABILA LA KISUKUMA