UTEKAJI WATOTO WATIKISA JIJI LA DAR

Stori: Makongoro Oging’
MUNGU
wangu! Lile sakata la utekaji na upoteaji wa watoto ambao wengi ni wanafunzi wa shule za msingi katika Jiji la Dar na kudaiwa linafanywa na watu walio kwenye magari aina ya Toyota Noah limeingia katika sura nyingine.
Wanafunzi wa shule ya msingi wakitoka madarasani baada kutokea kwa hali ya vurugu.
Safari hii, gari moja lilitupiwa mawe na dereva nusura kuuawa kufuatia kufika katika Shule za Msingi za Kombo na Mtakuja zilizopo Vingunguti, Dar kwa lengo la kuzungumza na walimu kuhusu mikopo lakini likahofiwa lilikwenda kuteka watoto.
Tukio hilo lilijiri Ijumaa iliyopita na kusababisha vurugu kubwa kati ya wazazi na walimu hali iliyowafanya maafande wa Kituo cha Polisi Buguruni kuwasili katika eneo la tukio ili kutuliza ghasia na kwanusuru walimu.
Mmoja wa walimu akiwa na wanafunzi hao.
UWAZI ENEO LA TUKIO
Gazeti hili lilifika eneo la tukio muda mfupi na kuwakuta walimu wakiwa chini ya ulinzi wa polisi ili wasishambuliwe na wazazi ambao walivamia shule wakidai kwamba watoto watatu walitekwa na watu wenye Noah jeusi.

SABABU YA VURUGU
Vurugu hizo zilizoanza saa nne asubuhi siku hiyo zilitokea baada ya gari moja jeusi aina ya Toyota Noah kufika shuleni hapo na kushambuliwa na wananchi wakidai kwamba ndilo linalotumika kuwatekea watoto wao shuleni hapo.

Baadhi ya wazazi na wananchi wakiwa wametanda eneo la Shule za Kombo na Mtakuja zilizopo Vingunguti, Dar.
Mmoja wa wazazi aliyejitambulisha kwa jina la Huma Selemani alisema Noah hilo la mikopo kwa walimu lililokuwa na vioo vyeusi lilihisiwa ni la utekaji baada ya jana yake (Alhamisi) ambapo gari kama hilo lilifika shuleni hapo na dereva kumuuliza mmoja wa wanafunzi sehemu ambapo mwanafunzi huyo akasema haijui.
Ilidaiwa kuwa, pamoja na denti huyo kusema haijui  sehemu hiyo walimchukua na kumuingiza ndani ya gari hilo ili kuondoka naye lakini mzazi mmoja aliona na kupiga kelele huku akilishambulia kwa mawe gari hilo hadi walipomshusha mwanafunzi huyo na wao kutimka.
Maafande wa Kituo cha Polisi Buguruni wakiwa eneo la tukio kutuliza ghasia.
WANAFUNZI WATOKA MADARASANI
Mayowe hayo yaliwafanya wazazi kuvamia shule hizo na kusababisha wanafunzi kutoka madarasani huku wengine wakiruka ukuta na kukimbilia majumbani na baadhi kwenda kusikojulikana.

Wazazi waliokuwa karibu na shule hizo walifika na kuwachukua watoto wao kisha kwenda nyumbani huku wengine wakitegemea msaada toka polisi ambao walipofika walifyatua risasi hewani kuwatawanya wananchi hao.
Walimu wakipandishwa gari kurudishwa makwao.
MANENO YA WALIMU
Hata hivyo, walimu wakuu wa shule hizo hawakupatikana mara moja lakini mwalimu mmoja ambaye hakupenda jina lake liandikwe gazetini alisema hakuna utekaji wa watoto shuleni bali baadhi ya watu wamekuwa wakivumisha habari hizo na hivyo kuwatia hofu watoto.

MADAI YA WATU
Baadhi ya watu walioongea na gazeti hili walisema kuwa, wana taarifa mbaya kwamba watekaji hao wakishawapata watoto huenda kuwaua ili kutwaa viungo vyao kwa ajili ya ushirikina wa kupata utajiri.

Baadhi ya walimu wakilindwa na maafande wasishambuliwe na wazazi waliovamie shuleni hapo.
UONGOZI WA MTAA
Mwenyekiti wa Serikali ya Mtaa wa Kombo, Jastin John Chiganga alipohojiwa alikiri kutokea kwa vurugu hizo hali iliyomfanya awaite polisi kutuliza ghasia lakini alisema kwa upande wa kutekwa watoto na gari aina ya Noah hajawahi kusikia.

“Shule ilibidi ifungwe, watoto waruhusiwe kutawanyika hadi hapo taarifa itakapotolewa. Hata hivyo, wazazi wameniomba kwamba kabla watoto wao hawajarejea shuleni hapo anatakiwa kiongozi wa juu, awe DC (mkuu wa wilaya) au yeyote afike kutoa tamko na kuweka mambo ili kuwatoa hofu wazazi na wanafunzi,” alisema mwenyekiti huyo.
Mwanafunzi Hadija Hansi (10) wa darasa la nne katika Shule ya Msingi Magomeni, Dar aliyepotea.
Polisi wa Buguruni waliokuwepo kwenye tukio hilo walisema hawana taarifa ya watu waliojeruhiwa au  kukamatwa bali zoezi la kudhibiti amani lilifanyika kwa uangalifu wa hali ya juu.
Wakati huohuo, wazazi wa mwanafunzi Hadija Hansi (10) anayesoma darasa la nne Shule ya Msingi Magomeni, Dar wanahaha kumtafuta mtoto wao huyo ambaye alitoweka katika mazingira ya kutatanisha ikidaiwa alitekwa na Noah.
Mfano wa gari la Noah linaloshukiwa kuhusika na utekaji wa watoto
Akizungumza na gazeti hili wiki iliyopita, Zena Amour ambaye ni mama mzazi wa mtoto huyo alisema mwanaye alipotea katika mazingira ya kutatanisha Septemba 30, mwaka huu wakati akicheza na wenzake na ameshamtafuta katika vituo vya polisi jijini kikiwemo cha Tandale TAND/RB/1059/2014 na hospitali zote bila mafanikio.

Chanzo:globalpublishers

Comments

Popular posts from this blog

PATA UKWELI KUHUSU MWANAMALUNDI, MTU WA MAAJABU ALIYEWAHI KUTOKEA KATIKA HISTORIA YA KABILA LA KISUKUMA