FAHAMU IBARA 28 ZA TUME YA WARIOBA ZILIZOONDOLEWA

Jaji Joseph Sinde Warioba.
Katiba Inayopendekezwa  ambayo inatarajiwa kupigiwa kura na wananchi Aprili 30, mwaka huu awali ilikuwa na Ibara 28 ambazo Tume ya Mabadiliko ya Katiba chini ya Jaji Joseph Sinde Warioba iliona zinafaa kuwemo lakini Bunge la Katiba chini ya Spika Samwel Sitta ikaona hazifai, hivyo kuzifuta.

Ibara zilizoondolewa zimeleta malalamiko kwa wananchi kwani zimeonekana zinafaa zikiwemo zinazowataka viongozi wa umma kutopokea zawadi kwa manufaa yao binafsi wala kufungua akaunti ya benki nje ya nchi pasipo sababu maalumu. Leo tunaendelea kuwaletea ibara hizo zilizofutwa ili nawe msomaji uone kama zilifaa kufutwa au la:
18.-(1) Kiongozi wa umma hatashiriki katika kufanya uamuzi wa jambo au shughuli yoyote ambayo ana masilahi nayo yeye binafsi, mwenza wake, mtoto wake, jamaa yake, rafiki au mtu yeyote wa karibu.

(2) Kiongozi wa umma hatazungumzia kitu chochote katika Baraza la Mawaziri, Bunge, Kamati au chombo kingine chochote rasmi ambacho ana masilahi nacho ya moja kwa moja au vinginevyo, isipokuwa tu kama atatoa taarifa ya mgongano huo wa masilahi katika chombo hicho.

(3) Itakuwa ni marufuku kwa kiongozi wa umma kushiriki katika uamuzi unaohusu kuongeza au kuboresha masilahi kwa namna yoyote ile yanayohusu wadhifa alionao na endapo atashiriki, basi masharti hayo mapya yataanza kutumika kwa kiongozi wa umma atakayekuja baada ya kiongozi husika kuondoka au kumaliza muda wa kukaa katika nafasi ya madaraka iliyompatia fursa ya kushiriki katika kuamua masilahi husika.

(4) Masharti ya ibara ndogo ya (3), hayatamhusu kiongozi wa umma ambaye kutokana na asili ya nafasi ya madaraka au aina ya kazi zake anapaswa kushiriki katika upangaji wa mishahara au maslahi mengine ya watumishi wa umma.

(5) Kiongozi wa umma hataruhusiwa kushika nafasi za madaraka zaidi ya moja au kutumikia mihimili ya dola zaidi ya mmoja kwa wakati mmoja.

19. Kiongozi wa umma hataruhusiwa kutumia au kuruhusu kutumika kwa mali yoyote ya umma, zikiwemo zilizokodishwa kwa serikali, kwa madhumuni ya kujipatia yeye binafsi au kumpatia mtu mwingine manufaa yoyote.
20.-(1) Bunge litatunga sheria itakayosimamia, pamoja na mambo mengine:

(a) utaratibu wa utwaaji wa mali za viongozi wa umma zilizopatikana kwa kukiuka sheria;
(b) utaratibu wa kumwajibisha kiongozi wa umma aliyekiuka maadili na Miiko ya Uongozi; na
(c) uanzishaji wa mitaala inayohusu Katiba, maadili na uraia, shuleni na vyuoni.
(2) Masharti yaliyoainishwa katika sehemu hii ya Sura ya Tatu yatatumika pia kwa watumishi wa umma baada ya kufanyiwa marekebisho stahiki.

63. Kwa ajili ya utekelezaji bora wa shughuli za Serikali ya Jamhuri ya Muungano na kwa ajili ya mgawanyo wa madaraka juu ya shughuli hizo baina ya vyombo vilivyotajwa katika Ibara ya 61, Serikali ya Jamhuri ya Muungano itakuwa na mamlaka juu ya mambo ya Muungano kama yalivyoorodheshwa katika Nyongeza ya Katiba hii. Nchi Washirika.

64.-(1) Kwa mujibu wa Katiba hii, Nchi Washirika ni Tanganyika na Zanzibar.
(2) Serikali ya Tanganyika itakuwa na mamlaka juu ya mambo yote yasiyo ya Muungano yanayohusu Tanganyika.
(3) Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itakuwa na mamlaka juu ya mambo yote yasiyo ya Muungano yanayohusu Zanzibar.

(4) Nchi Washirika zitatekeleza majukumu yao kwa kuzingatia masharti ya Katiba hii na Katiba zao.
(5) Nchi Washirika zitakuwa na hadhi na haki sawa ndani ya Jamhuri ya Muungano na zitatekeleza majukumu yao kwa mambo yote yasiyo ya Muungano katika mamlaka ya Nchi Washirika kwa mujibu wa masharti yatakayowekwa na Katiba za Nchi Washirika.

67.-(1) Kila Nchi Mshirika itateua Waziri Mkaazi atakayeratibu na kusimamia mahusiano baina ya Serikali za Nchi Washirika na kati ya Serikali ya Nchi Mshirika na Serikali ya Jamhuri ya Muungano.
(2) Mawaziri Wakaazi watakuwa na ofisi zao na watafanya kazi wakiwa Makao Makuu ya Serikali ya Muungano.Itaendelea wiki ijayo.

Comments

Popular posts from this blog

PATA UKWELI KUHUSU MWANAMALUNDI, MTU WA MAAJABU ALIYEWAHI KUTOKEA KATIKA HISTORIA YA KABILA LA KISUKUMA