MGOMBEA URAIS UKAWA YUPO CCM, SIRI IMEVUJA

 
Steven Wassira.
Habari za kuaminika kutoka ndani ya kambi ya Ukawa inayoundwa na vyama vya Chadema, Cuf, NCCR-Mageuzi na NLD, zinasema kwa muda mrefu, mgombea huyo amekuwa katika mazungumzo na chama kimoja kikubwa cha upinzani Tanzania Bara na kwamba wameshakubaliana mambo makubwa muhimu ya kuzingatiwa ili kukamilisha mchakato huo.

Inadaiwa kuwa awali mazungumzo yalikuwa kati ya Chadema na kada huyo wa CCM ambaye ni miongoni mwa viongozi waliopewa adhabu na kamati kuu (CC) ya chama hicho kwa kosa la kuanza mapema kampeni za kuwania kiti hicho, wakifikia makubaliano kuwa endapo chama chake kitamuengua katika kuwania nafasi hiyo, basi afanye hivyo kupitia chama hicho lakini kwa sharti la kugawana vyeo yeye na wafuasi atakaoondoka nao.

“Kambi ya kada huyo ina hofu ya mzee wao kukatwa kutokana na mizengwe inayosukwa na wapinzani wake ndani ya chama. Kwa kuwa ni lazima mtu wao awanie urais, basi wameamua kuweka mbadala. Vikao vimefanyika na walifikia hatua nzuri kwa sababu wanaamini endapo mgombea huyo ataondoka CCM na kujiunga kule wana uhakika wa kupata kura nyingine zikitoka hata kwa wafuasi wa chama hicho tawala,” alisema mtoa habari wetu.
Inadaiwa kuwa awali, kulikuwa na hofu ya mpango huo kuharibika baada ya Chadema kujiunga na vyama vingine vya upinzani na kuunda Ukawa, ambao wametangaza kumweka mgombea mmoja atakayekubaliwa na pande zote, lakini imeelezwa kuwa mazungumzo yanaendelea na upo uwezekano mkubwa wa mpango huo kukubaliwa na viongozi wa vyama vingine kutokana na nguvu kubwa ya ushawishi iliyonayo chama hicho.

“Kwa jinsi alivyo na wafuasi wengi ndani ya CCM na vuguvugu la mabadiliko linalosubiri uchaguzi wa mwaka huu, kuna uwezekano mkubwa wa kushinda kupitia Ukawa. Kada huyo ametaka kuwekewa nafasi kadhaa katika serikali itakayoundwa na makubaliano yamefikiwa juu ya vyeo ambavyo watu wa Ukawa watapata katika serikali inayotarajiwa kuundwa,” kilisema chanzo hicho.

Kwa mujibu wa mtoa habari wetu, baadhi ya nafasi ambazo Ukawa wametaka kupewa ni ile ya mgombea mwenza (atakayekuwa makamu wa rais), waziri mkuu, wizara ya fedha, wizara ya sheria, wizara ya mambo ya ndani, wizara ya ulinzi, wizara ya nishati na madini, wizara ya ujenzi na uchukuzi pamoja na nyingine nyeti ambazo zinadaiwa kuwa ndiyo uti wa mgongo wa uchumi wa nchi.

“Wanaamini wakizikamata wizara hizo, basi wanao uwezo wa kubadilisha mambo na hivyo kuonesha tofauti kati ya uongozi wao na ule wa CCM. Ninavyokueleza hivi, vikao bado vinaendelea kwa sababu kila upande unataka kujiridhisha kabla ya kufikia makubaliano rasmi,” kilisema chanzo hicho.
Juzi, Uwazi Mizengwe lilimtafuta Naibu Katibu Mkuu wa Chadema Tanzania Bara, John Mnyika kupitia simu yake ya mkononi na kumuuliza kuhusu mipango hiyo lakini alikataa katakata kuwepo kwa suala hilo akidai ni uvumi ambao hauna ukweli wowote.

“Huo uvumi hauna ukweli, mgombea wa Ukawa atatoka Ukawa. Wananchi wana imani na Ukawa na siyo mtu kutoka chama kilichoshindwa kujivua magamba ya ufisadi na kuwa chama cha mafisadi,” alisema Mnyika ambaye pia ni mbunge wa Ubungo kwa tiketi ya Chadema.

Alipoulizwa kama Ukawa watakuwa tayari kumpokea kada wa CCM mwenye wafuasi wengi kwa kigezo cha kuongezewa kura katika uchaguzi huo na kumpa nafasi ya kuwania urais, Mnyika alisema milango ipo wazi kwa kiongozi yeyote mwenye maono na maadili ambaye atakuwa tayari kumuunga mkono mgombea atakayeteuliwa na Ukawa, siyo mwenye uzoefu wa ufisadi na uongozi mbovu.

“Tayari Ukawa ina wafuasi wengi ambao wakiungana na wananchi wengine wasio na vyama lakini wapenda mabadiliko wanatosha kuiondoa CCM madarakani, lakini kama yupo mwenye maono na maadili aliye tayari kujiunga na Ukawa toka CCM ili kuongeza kura za mabadiliko aje, lakini nasisitiza, awe na uadilifu na uwezo siyo uzoefu wa ufisadi.”

Kwa upande wake, Katibu wa Itikadi, Uenezi wa Halmashauri Kuu ya CCM, Nape Moses Nnauye alipoulizwa juu ya suala hilo alipuuza na kusema ni porojo za mtaani ambazo CCM haishughuliki nazo.

Makada wa CCM wanaotajwa kuwa na nguvu katika chama hicho ambao pia wanatumikia adhabu ya kuanza kampeni mapema ni pamoja na Emanuel Nchimbi, Edward Lowassa, William Ngeleja, January Makamba, Steven Wassira na Bernard Membe. Wengine ambao hawako kwenye adhabu ni Mizengo Pinda, Hamis Kingwangalla na Lazaro Nyalandu.

CREDIT: Na Ojuku Abraham/ UWAZI MIZENGWE

Comments

Popular posts from this blog

PATA UKWELI KUHUSU MWANAMALUNDI, MTU WA MAAJABU ALIYEWAHI KUTOKEA KATIKA HISTORIA YA KABILA LA KISUKUMA