Watishia kufunga viwanda vya bia na vya pombe kali


Watengenezaji wa bia na vinywaji vikali, wametishia kufunga baadhi ya viwanda iwapo Serikali haitaipunguza ongezeko la kodi la asilimia 20 iliyolipishwa kinyume na tozo ya asilimia 10 iliyopitishwa na Bunge.

Uamuzi huo umekuja baada ya wenye viwanda vya vinywaji hivyo kubaini kuwa Muswada wa Sheria ya Fedha wa mwaka 2014/15 uliotolewa Julai 11, mwaka huu, unataja kuwa kodi kwa bidhaa hizo itakuwa asilimia 20.
Akizungumza jana, mwakilishi wa wenye viwanda nchini, David Mgwassa alisema uamuzi wa kupandisha kodi kinyemela umewaacha njiapanda wenye viwanda kwa kuwa hawajui walipe kodi ipi kati ya asilimia 10 au 20 na kwamba, iwapo Serikali haitapunguza, watafunga baadhi ya viwanda ili kumudu ongezeko hilo jipya la kodi.
“Kila kampuni inafanya utafiti ili kufunga viwanda vyote na kubaki na kimoja kikubwa kitakachopunguza gharama. Pia ikumbukwe kuwa kuna viwanda vilijengwa kwa lengo la kuja kubinafsishwa, hivyo wengi watakosa ajira. Wawekezaji wana wasiwasi kama Tanzania ni sehemu nzuri kuwekeza tena.
“Kodi ya mwaka 2014 ni ipi? Viwanda vilipanga bei kulingana na asilimia 10, lakini Muswada wa Sheria ya Fedha unasema kodi hiyo imeanza rasmi kutoka Julai 1, mwaka huu, tutafilisi viwanda,” alisema Mgwassa.
Pia alihoji: “Kwa nini Bunge lijadili na kupitisha kodi asilimia 10 halafu muswada useme asilimia 20. Ni nani anayemtania mwenzake?”
Alisema iwapo mahitaji ya bidhaa hizo yatapungua nchini, kampuni zinazomiliki viwanda vya vinywaji zitalazimika kupunguza uzalishaji.
Alisema viwanda vya bia na vinywaji vikali vinapambana na ushindani mkali kutoka bidhaa za nje zinazoingia nchini kinyume cha sheria, jambo linaloweza kuufanya uchumi ukashuka iwapo hali hiyo haitadhibitiwa.

chanzo: Mwananchi.

Comments

Popular posts from this blog

PATA UKWELI KUHUSU MWANAMALUNDI, MTU WA MAAJABU ALIYEWAHI KUTOKEA KATIKA HISTORIA YA KABILA LA KISUKUMA