MADAKTARI NCHINI TANZANIA WATANGAZA MGOMO WIKI MBILI ZIJAZO.

Madaktari wakiwa Kazini.
MADAKTARI nchini wametishia kuanza mgomo mkali wiki mbili zijazo, iwapo serikali itashindwa kuyapatia ufumbuzi madai yao ya msingi, ikiwemo nyongeza ya mshahara.

Habari kutoka ndani ya kikao kilichoitishwa jana jijini Dar es Salaam na viongozi wa Chama cha Madaktari Tanzania (MAT), zimedai kuwa serikali imeyachukulia kisiasa madai yao.

Kikao hicho kililenga kujadili ripoti iliyotolewa na kamati iliyoundwa na Rais Jakaya Kikwete ya kushughulikia madai ya madaktari.

Madaktari waliikosoa ripoti hiyo kwa madai kuwa imeweka pembeni ushauri wa kitaalamu na badala yake umejaa siasa zisizotekelezeka.

Mmoja wa wachangiaji katika mkutano huo ambaye jina lake halikuweza kujulikana mara moja, alisema kuwa hakubaliani na ripoti hiyo kwa kuwa haionyeshi uhai wa madaktari na “Haya ni majibu ya kihuni, hivi unaweza kutuambia kuwa madai yetu yatatekelezwa katika bajeti ya mwaka 2013/2014… sisi tupo katika hatari ya kupata maambukizi, leo serikali inadai itatupa chanjo kwa awamu, haya ni majibu ya kisiasa, nadhani sasa imetosha tuweke dhana zetu chini,” alisema mchangiaji huyo.

Mchangiaji mwingine alisema kuwa, kutokana na kuanza kwa vikao vya Bunge, wanaamua kutoa wiki mbili ili kuhakikisha madai yao yanatekelezwa, na iwapo itashindikana, hawana budi kuweka mikakati ikiwa ni pamoja na kuwashirikisha wenzao waliopo mikoani kwa lengo la kuanzisha mgomo usio na kikomo.

Aliongeza kuwa, wamekubaliana kutohofia kufukuzwa kazi kama ambavyo wanatishiwa na watawala kila wanapofanya migomo.

Alisema serikali inashindwa kuwathamini madaktari na kuipa siasa umuhimu, akitolea mfano mkutano wa jana wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) ambao anaufananisha na kumfufua ngamia aliyekufa jangwani.

Wakizidi kuchangia, walisema serikali kwa sasa imeshaharibikiwa na haiwezi kutekeleza jambo lolote ndiyo maana haithamini michango ya madaktari.

“Viongozi wetu wamevimbiwa na ufisadi, kila kukicha badala ya kuangalia njia sahihi za kutatua matatizo ya wananchi wenyewe wanafikiria ufujaji wa rasilimali,” alisema mmoja wa madaktari hao.

Akizungumza na waandishi wa habari kuhusu maazimio ya kikao hicho, Rais wa MAT, Dk. Namala Mkopi alisema kuwa walikutana na madaktari hao kwa ajili ya kupata mrejesho juu ya kamati iliyoundwa na Rais Kikwete kufuatilia madai ya madaktari.
Rais wa MAT, Dk. Namala Mkopi

Dk. Mkopi alisema kuwa, katika mrejesho huo madaktari hao wameikataa ripoti hiyo na kuwataka viongozi hao kuirudisha taarifa hiyo kwa serikali na kuipa wiki mbili.

“Wameikataa ripoti na wametutaka kuijibu taarifa hiyo na kuirudisha serikalini…nasi kama viongozi tutatekeleza hilo. Wametangaza mgogoro na serikali na baada ya wiki hizo mbili wataingia katika mgomo usio na kikomo,” alisema.

Madai ya madaktari hao ambayo serikali imeeleza kushindwa kuyatekeleza katika mwaka huu wa fedha hadi katika bajeti ya mwaka 2013/2014 ni pamoja na kuwalipa posho, ikiwamo za kulala kazini walizodai tangu mwaka 2004 ambazo hazijawahi kubadilika kutoka kiwango cha sasa cha sh 10,000 licha ya  mwongozo wa serikali kuelekeza walipwe kwa nusu ya fedha ya mkoa husika.

Madai mengine ni kulipwa posho kwa wale wanaofanya kazi katika mazingira hatarishi yanayoweza kuwaambukiza magonjwa na kuwasababishia athari mbalimbali, ili iwatie morali.

Pia wanadai kulipwa posho ya kufanya kazi katika mazingira magumu, kupata posho kwa ajili ya usafiri au mkopo wa gari, kupatiwa nyumba za kuishi, kuboreshewa mishahara yao, posho ya uchunguzi wa maiti na kupatiwa bima ya afya wao na familia zao.

Huu unaweza kuwa ni mgomo wa tatu iwapo utatekelezwa baada ya ule uliotokea Januari ambao ulidumu kwa takriban wiki mbili na wa pili uliotokea Machi mwaka huu.
Madaktari wakiwa kazini.

Migomo hiyo ilisababisha baadhi ya wananchi kupoteza maisha na wengine kupata majeraha ya kudumu kabla ya serikali kuingilia kati.

Waziri Mkuu Mizengo Pinda, alitangaza kusimamishwa kazi kwa aliyekuwa Mganga Mkuu wa Serikali, Deo Mtasiwa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya, Blandina Nyoni.
Waziri Mkuu wa Tanzania Mizengo Pinda

Pia serikali iliunda timu ya kushiriki kwenye meza ya majadiliano na madaktari, lakini hata hivyo suluhu haikupatika na hivyo kurejea kwenye mgomo mwingine.

Mgomo wa pili ulisitishwa baada ya Rais Jakaya Kikwete kukutana na viongozi wa MAT na kuwaahidi kushughulikia madai yao kwa kuunda tume yenye wajumbe wa pande hizo mbili.

CHANZO:TANZANIA DAIMA.

Comments

Popular posts from this blog

PATA UKWELI KUHUSU MWANAMALUNDI, MTU WA MAAJABU ALIYEWAHI KUTOKEA KATIKA HISTORIA YA KABILA LA KISUKUMA