WATOTO WATAKIWA KUPEWA HAKI ZAO

Na Shomari Binda
Musoma,
Jamii imetakiwa kuzielewa na kuzithamini haki mbalimbali zinazohusiana na kutakikana kwa watoto ikiwa ni lengo la kumwezesha mtoto katika kufanikisha malengo ya millenia kwa mwaka 2015



Hayo yalisemwa leo na afisa Maendeleo ya jamii Manispaa ya Musoma Janeth Mafipa alipokuwa akifungua warsha juu ya haki za watoto iliyofanyika katika ukumbi wa Dayosisi ya Anglikana Mjini Musoma.

Alisema ni jukumu la jamii katika kuwapa watoto haki zao za msingi ambazo zimeainishwa sehemu mbalimbali zikiwemo Sheria na miongozo ikiwa ni lengo la kuiandaa jamii yenye maadili na makuzi yalio bora kama ambavyo jamii nyingine inahitaji.

Janeth alisema jamii haiwezi kuendelea kama itapuuza haki za watoto ambazo wanazihitaji na kutamkwa katika matamko hivyo ni vyema jamii na taasisi mbalimbali za Serikali na watu binafsi wakaziheshimu haki za watoto na kuzitekeleza ipasavyo bila kumuathiri mtoto.

Katika warsha hiyo ambayo inawakutanisha wadau mbalimbali kutoka Mkoani Mara pamoja na mashirika yasiyo ya kiserikali inalenga kuikumbusha jamii juu ya kuheshimu na kuzilinda haki za watoto kama njia ya kuzitambua sheria mbalimbali za kimataifa ambazo nchi imeridhia.

Alisema kuwa jamii ya sasa imekuwa haiwajibiki ipasavyo katika kuzitekeleza haki hizo na kupelekea kuibuka kwa watoto wa mitaani na kukosa malezi yalio bora na hivyo kupotezaa haki za watoto za msingi wanazohitaji.

Mratibu wa Umoja wa Maendeleo ya Bukwaya (UMABU) ambao ndio waandaaji wa warsha hiyo Bulunde Ndago alisema kuwa madhumuni ya warsha hiyo ni kupitia majadiliano na kuelimisha maana ya haki za watoto kwa wadau wa Maendeleo ya mtoto ili kurahisisha utendaji wa shughuli zao za kuwaendeleza watoto.

Alisema warsha hiyo ya siku tatu imeandaliwa na Shirika la UMABU ambalo linafadhiliwa na Shirika la Terre-Des Hommes kutoka nchini Uholanzi linajishughulisha katika masuala ya elimu,maji na afya katika vijiji 15 Mkoani Mara.

Mbali na hivyo pia UMABU inajishughulisha na shughuli za uzalishaji mali,utunzaji wa mazingira,masuala ya vvu/ukimwi katika eneo la Bukwaya katika Halmashauri ya Musoma Vijijini na kwa sasa inao mpango wa kutoa huduma zake katika Mkoa mzima wa Mara.

Comments

Popular posts from this blog

PATA UKWELI KUHUSU MWANAMALUNDI, MTU WA MAAJABU ALIYEWAHI KUTOKEA KATIKA HISTORIA YA KABILA LA KISUKUMA