CHADEMA YAITEKA MTWARA

chadema mtwara  
Aliekuwa Mbunge wa Arusha Mjini, Mh Godbless Lema akihutubia maelfu ya wananchi wa Mtwara katika Viwanja vya Mashujaa jana. CHADEMA wako mikoa ya kusini mwa Tanzania kwa ziara ya kuimarisha chama hicho katika maeneo hayo na pia kuutanzaza mapango wao mpya wa kuwashirikisha wananchi katika shuguli za chama (Movement for Change-M4C) kuanzia jana hadi Juni 11, 2012
*********
DHANA ya kuwa mikoa ya kusini ni ngome ya Chama cha Mapinduzi jana ilifutika vichwani mwa wakazi wa mikoa hiyo, baada ya umati mkubwa kujitokeza, kuulaki msafara wa viongozi na hatimaye kuhudhuria mkutano mkubwa wa hadhara uliofanyika katika viwanja vya Mashujaa, mkoani Mtwara. 

Msafara huo wa kitaifa ukiongozwa na Mwenyekiti Freeman Mbowe, ulipata mapokezi ya vijana wakiwa katika msafara wa pikipiki magari na baiskeli karibu na daraja la Mikindani na kuelekea katika uwanja wa Mashujaa ambapo umati mkubwa wa watu ulifurika kupita kiasi. 

Akihutubia katika mkutano huo Mwenyekiti wa CHADEMA Taifa Freeman Mbowe alisema ameshajiandaa kisaikolojia kufa kwa ajili ya kutetea haki na kwamba wananchi wasiogope kupigania haki zao. 

Alisema ikitokea akafa akiwa katikati ya mapambano waliobaki wasihuzunike bali wahakikishe huo ndiyo unakuwa mwanzo wa ukombozi. 

“Nikifa katika mapambano haya uinueni mwili wangu uwekeni pembeni na kisha endeleeni na mapambano kwa kuwa haya si ya Mbowe peke yake bali ni ya Watanzania wote,” alisema Mbowe.
Aliwaambia wakazi wa Mtwara kuwa hawakwenda pale kutafuta jimbo au kata bali kuleta ukombozi wa kweli kwa kuwa ni wajibu wa kila Mtanzania kuhakikisha nchi inakombolewa. 

Akizungumzia kuhusu udini, Mbowe alisema viongozi wa serikali wanaotumia udini, ukabila na ukanda kuwagawa watu wamekata tamaa ya kuwatumikia. 

Alisema kuwa kwa hali ilivyo itakuwa ni hatari zaidi kwa ustawi wa Tanzania kama hata tone moja la mafuta yatapatikana huku nchi ikiwa inaongozwa na serikali ya CCM kwa kile alichodai tayari wamemwaga damu kwa tamaa ya mali katika rasilimali zilizokwishaanza kupatikana. 

Naye Katibu mkuu wa CHADEMA, Dk. Willibrod Slaa, aliwataka polisi kuacha kuwanyanyasa raia na kueleza hata yanayotokea Zanzibar kwa sasa ni udhaifu wa Rais Jakaya Kikwete wa kutaka kuzuia watu wasitoe maoni. 

Alisema hatua ya kuwataka watu wasijadili suala la Muungano wakati unawagusa haiwezi kukubalika na kwamba polisi wawe na akili ya kuambiwa na kisha kuchanganya na zao kwa ajili ya maslahi ya Tanzania. 

“Kikwete amesababisha hali hii ya Zanzibar, maana hakukuwa na haja ya kumkamata mtu aliyekuwa anatoa maoni juu ya mustakabali wa nchi yake,” alisema Dk. Slaa. 

Kuhusu bajeti ya 2012/2013 Dk. Slaa alitaka isimamishwe na mishahara ya wafanyakazi iboreshwe. 

Kuhusu korosho, Dk. Slaa alisema wakazi wa Mtwara wanafanywa maskini huku korosho zao zikienda kutoa ajira kwa wananchi wa India na wajanja wachache wa hapa nchini. 

“Tanzania haitakombolewa bila mikoa ya kusini kuwa huru, tunataka mtuunge mkono katika kila hatua ili tuchukue nchi 2015,” alisema Dk. Slaa. 

Mnyika adai Bunge ni Kanyaboya
Mbunge wa Ubungo John Mnyika akihutubia umati huo alisema Bunge la Tanzania halina nguvu ya kuiwajibisha serikali na kama litafanya hivyo Rais anaweza kuwatimua wabunge wote. 

Alisema hali hiyo inachangiwa kwa kiasi kikubwa na Katiba liyopo ambayo alisema ni lazima Watanzania wajitokeze na kuingiza mambo ya msingi wakati wa kutoa maoni. 

Aliongeza wakazi wa Mtwara wanashindwa kufaidika na gesi iliyoko mkoani humo pamoja na kukosa uwezo wa kumiliki ardhi kwa amendeleo yao. 

Mawazo abeba silaha
Aliyekuwa diwani wa CCM kata ya Arusha Alphonce Mawazo aliwaambia wakazi wa Mtwara kuwa mabadiliko ya kweli huanza kwenye akili na mtu akishafungua akili kila kitu chake kitaenda kwa ufasaha na kuwa huru. 

Huku akishangiliwa na umati wa watu uwanjani hapo Mawazo alisema wameenda Mtwara wakiwa na silaha za nguvu ya umma, na kuwataka wasitengane katika kutafuta mabadiliko ya kweli, na kuachana na waliowasaliti kwa kuwaingiza katika maisha magumu.
Aliwaeleza wakazi wa Mtwara kuwa wamefungwa na minyororo ya umaskini na kwamba minyororo hiyo ni mibaya kwa mustakabali wa maisha yao kuliko hata minyororo ya chuma waliyokuwa wakifungwa watumwa enzi za ukoloni 

Millya: CCM imeshaanza  kuaga
Kwa Upande wake aliyekuwa Mwenyekiti wa UVCCM Mkoa wa Arusha James Millya alisema harakati zilizoanzishwa na CCM hivi karibuni kutaka nafasi ya mgombea urais ihojiwe  mahakamani ni baada ya kugundua mwaka 2015 hawatakuwa na nafasi ya kushinda hivyo kimbilio lao ni mahakamani. 

“CCM wanatuaga na mkitaka kuamini hilo sasa wameanza kutaka nafasi ya urais ihojiwe mahakamni kwa kuwa huko ndiko kimbilio lao lililobaki kwa sasa,” alisema Millya. 

Alisema CCM inaichukia CHADEMA kwa kuwa inataka uhakika wa maisha hata kwa mtoto wa maskini ambaye hajui hatma yake ya maisha kwa siku zijazo. 

Aliongeza kuwa ni wakati muafaka sasa kwa Watanzania kuachana na watu waliowasaliti kwa kushindwa kusimamia wajibu waliokabidhiwa. 

Habari na Tanzania Daima, Mei 29. 2012

Comments

Popular posts from this blog

PATA UKWELI KUHUSU MWANAMALUNDI, MTU WA MAAJABU ALIYEWAHI KUTOKEA KATIKA HISTORIA YA KABILA LA KISUKUMA