Waziri Akumbana Na Madudu Maliasili

 WAZIRI mpya wa Maliasili na Utalii, Balozi Khamis Kagasheki, ameelezea kushtushwa kwake na ubadhilifu wa kutisha ulioko katika wizara hiyo, Idara ya Wanyamapori unaodaiwa kufanywa na baadhi ya watendaji wake.
 
Akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya kuzindua Bodi ya Ushauri ya Wizara ya Wakala wa Huduma za Misitu (TFS) jijini Dar es Salaam, jana, waziri huyo alisema idara hiyo inanuka kwa uozo unaotokana na wizi na ubadhilifu mkubwa ambao umeleta hasara kwa taifa.
 
Kagasheki alidai idara hiyo inaongoza kwa madudu ya kutisha, na ametangaza kuchukua hatua za haraka dhidi ya watendaji wanaotuhumiwa kuhusika na ubadhilifu huo mkubwa haraka iwezekanavyo, akidai fedha zilizotafunwa na wajanja hao ni nyingi.
 
“Jamani Idara ya Wanyamapori ina fedha nyingi, lakini zinaliwa na watu kwa maslahi binafsi, na kama fedha hizo zingekuwa zinapelekwa serikalini kama inavyohitajika, nchi hii kwa sasa ingefika mbali, mimi naogopa hata kutaja kiasi cha fedha hapa hadharani,” alisema.
 
Mbali na ufujaji huo, Balozi Kagasheki amekiri kuwa, usafirishaji wanyamapori nje ni mkubwa mno licha ya serikali kusitisha biashara hiyo.
 
Alisema uchunguzi wa haraka umebaini kuwa, biashara ya kusafirisha wanyama pori inafanywa kati ya wafanyabiashara wa ndani na baadhi ya watendaji, ambao hawajali na wanaonekana kutumia kila mbinu kuifanikisha.
 
Hata hivyo, katika hali iliyotarajiwa, Balozi Kagasheki alionesha hofu yake ya kukabiliana na wafanyabiashara na baadhi ya maafisa wa wizara hiyo, kiasi cha kuomba msaada kutoka taasisi nyingine, vikiwemo vyombo vya habari kusaidia kupambana na ‘genge’ la wabadhilifu hao.
 
“Katika idara kunahitaji usaidizi maana hapa ni vita, na hata ninyi waandishi nafikiri mnaweza tukasaidiana kwa kuwa najua mtakuwa mnawajua sana wafujaji. Kuwaondoa hawa ni kutangaza vita,” alisema.
 
Kutokana na hali hiyo, alisema atavunja uongozi wa idara hiyo na kuunda upya haraka iwezekanavyo, ingawa ni mapema sana kufanya hivyo. Soma Zaidi http://www.freemedia.co.tz

Comments

Popular posts from this blog

PATA UKWELI KUHUSU MWANAMALUNDI, MTU WA MAAJABU ALIYEWAHI KUTOKEA KATIKA HISTORIA YA KABILA LA KISUKUMA